China yafungua tena biashara na Afghanistan

Ndege ikiruka kutoka uwanja wa ndege wa Kabul, Afghanistan.

China imefufua tena biashara za moja kwa moja kwa njia ya ndege na Afghanistan katika juhudi ya kulisaidia taifa hilo lililoathiriwa na vita vya muda mrefu pamoja na kuwezesha viongozi wapya wa Taliban kukabiliana na matatizo  ya kiuchumi na kibinadamu yanayoendelea kushuhudiwa. 

Ndege ya mizigo iliyokuwa imebeba tani 45 za mbegu za Pine Jumapili imeondoka kwenye uwanja wa ndege wa Kabul kuelekea kwenye masoko ya China, ikiashiria ukurasa mpya wa kibiashara kati ya mataifa hayo tangu Taliban kukamata serikali mwezi Agosti.

Msemaji wa serikali ya Taliban Bilal Karimi ameiambia VOA kwamba wanatumai shughuli za kibiashara zitaendelea kuimarika kati ya taifa lake na China.

Amesema kwamba hatua hiyo ni kufuatia mashauriano ya hivi karibuni kati ya Kabul na Beijing, akiongeza kwamba wanapiga hatua kuelekea kwenye ushirikiano zaidi katika siku zijazo. China ndilo soko kubwa zaidi la mbegu za Pine kutoka Afghanistan.

Wakati biashara hiyo ilipofunguliwa awali mwaka 2018, wataalamu walikisia kwamba Afghanistan ingepeleka tani 23,000 za bidhaa hiyo kila mwaka nchini China, wakati ikijipatia takriban dola milioni 800.