China kutoa chanjo za Covid-19 Africa

Mwanaume apokea chanjo ya Covid-19 aina ya Sinovac kutoka China.

China Alhamisi imesema kuwa inatoa chanjo za Covid-19 kwa karibu mataifa 40 ya kiafrika ikieleza hatua hiyo kuwa ya kibinadamu wakati baadhi wakiona kana kwamba ni mwendelezo wa kile kinatajwa kuwa diplomasia kupitia utoaji wa chanjo.

Kwa mujibu wa shirika la habari la AP, waziri wa mambo ya kigeni wa China Wu Peng, ameambia wanahabari kwamba china imetoa misaada ya kuuza chanjo hizo kwa bei nafuu kwa mataifa hayo.

China imesema kuwa imechukua msimamo tofauti na baadhi ya mataifa yaliosema kuwa yangetoa chanjo kwa mataifa mengine baada ya kukamilisha kutoa chanjo kwa watu wake ikionekana kulenga Marekani.

Licha ya Marekani kulaumiwa na baadhi ya mataifa kwa kutopeleka chanjo kwa mataifa mengine, Rais Joe Biden Jumatatu ameahidi kutoa dozi milioni 20 katika muda wa wiki sita zijazo na kufikisha jumla ya chanjo zilizotolewa na Marekani kufikia sasa kuwa milioni 80.

Hata hivyo haijafafanuliwa ni mataifa yapi yatakayopokea chanjo hizo. Dozi hizo zinatarajiwa kutoka kwa makampuni ya kutengeneza dawa ya Marekani kama vile Pfizer, Moderna na Johnson & Johnson.

Mtayarishaji- Harrison Kamau