Baraza la Seneti laamua kuwaita mashahidi kesi ya Trump

Baraza la Seneti likiendelea na kikao chake kusikiliza kesi ya kumshtaki Rais wa zamani Donald Trump Washington, Saturday, Feb. 13, 2021. (Senate Television via AP).

Baraza la Seneti la Marekani limepiga kura na kupitisha kuwa mashahidi waitwe kwenye kesi ya kumshtaki Rais wa zamani Donald Trump.

Hatua hiyo imefikiwa katika kikao chake Jumamosi asubuhi ambapo Maseneta Warepublikan watano na Maseneta Wademokrat 50 walikubaliana kuwaita mashahidi. Lakini Maseneta Warepublikan 45 walipinga hatua hiyo.

Siku ya Ijumaa, mawakili wa Trump walikamilisha utetezi wao wakikanusha tuhuma kwamba alisaidia kuchochea shambulizi la hatari lililofanywa na genge ndani ya Bunge la Marekani Januari 6.

Mawakili wa Trump wameieleza kesi hiyo ina ushawishi wa kisiasa na kinakwenda kinyume cha katiba.

“Ni kama zile nyingine za kumtafuta mchawi zenye ushawishi wa kisiasa wa mrengo wa kushoto umejihusisha nazo katika miaka minne iliyopita, kesi hii ya kumshtaki imekosa ukweli, ushahidi na maslahi ya watu wa Marekani", amesema wakili wa Trump Michael van der Veen.

Mawakili wa Trump waliwasiliisha utetezi wao kwa saa tatu Ijumaa, wakichgua kutotumia saa 16 walizokuwa wamepangiwa.

Mawakili wa Trump wamewaambia maseneta kuwa rais wa zamani alikuwa na kila haki kuhoji kushindwa kwake katika uchaguzi dhidi ya Rais Joe Biden na kuwa hotuba ya Trump ya dakika 70 dakika kadhaa kabla ya uvamizi ndani ya Bunge la Marekani Januari 6 haikuwa ni uchochezi kwa ghasia hizo.

Waendesha mashtaka katika kesi hiyo walisema Alhamisi kuna ushahidi “ wa wazi na wakutosha” kuwa Trump alichochea uvamizi wa Capitol kwa kupeleka genge la wafuasi wake kuvamia Bunge la Marekani mwezi uliopita ili kuwashambulia wabunge wakati wakirasmisha kuwa alishindwa katika uchaguzi wa Novemba dhidi ya hasimu wake Mdemokrat Joe Biden.