Mahakama Somalia yatoa adhabu ya kifo kwa Askari aliyemuua Siraji

Abbas Abdullahi Sheikh Siraji.

Mahakama ya kijeshi Mogadishu Jumatatu imetoa hukumu ya adhabu ya kifo kwa askari wa serikali baada ya kupatikana na hatia ya kumuua waziri wa ujenzi wa Somalia, Abbas Abdullahi Sheikh Siraji.

Hassan Ali Shuute, mwenyekiti wa mahakama hiyo ya kijeshi amesoma hukumu hiyo, akisema kuwa hukumu hiyo dhidi ya Ahmed Abdullahi Abdi (Aided), 29, imekuja baada ya mahakama ya kijeshi kufikia uamuzi ambao ulifikiwa baada ya uchunguzi uliochukuwa miezi kadhaa.

“Baada ya uchunguzi wa muda mrefu na ushahidi kadhaa kutolewa kuhusiana na mauaji ya waziri, mahakama hiyo imejiridhisha kuwa mtuhumiwa alikusudia kupiga risasi iliyosababisha kifo cha waziri, na hivyo basi na yeye anatakiwa aonje adhabu kama hiyo,” Shuute amesema.

Siraji, mwenye umri wa miaka 31, ambaye alikuwa ndiye mwanasiasa mdogo katika baraza la mawaziri la Somalia alipigwa risasi ya usoni karibu na ikulu ya rais, mwezi Mei mwaka huu.

Walioshuhudia tukio hilo wameiambia VOA wakati Siraji alipopigwa risasi kutoka kwenye gari ambayo Mkaguzi Mkuu Nur Jimale Farah alikuwa ndani yake. Farah alifukuzwa kazi mara moja.

Makundi ya haki za binadamu aghlabu yamekuwa yakiishutumu mahakama ya serikali ya kijeshi kwa kutoa hukumu kama hizo za kifo, ambazo hutekelezwa mbele ya umma kwa mtu kupigwa risasi, bila ya mtuhumiwa kupewa nafasi ya utetezi au kushtakiwa kwa mujibu wa sheria, lakini Shuute anasema kuwa mawakili wanane walihusishwa katika kesi hii na mtuhumiwa anaweza kukata rufaa.