Watu 8 wauwawa katika shambulio la kutumia gari New York

Baiskeli zilizogongwa wakati wa shambulizi la New York siku ya Jumanne Oktoba 30.

Mamia ya wakazi wa New York washiriki katika gwaride la kuadhimisha siku ya wafu saa chache baada ya dereva wa lori dogo kuwagonga na kuwauwa watu 8 na kuwajeruhi zaidi ya 12 siku ya Jumanne.

Meya wa jiji la New York Bill de Blasio akizungumza na waandishi habari alisema "kufutana na habari tulizonazo kwa wakati huu, hili ni tukio la kigaidi, na hasa ni kitendo cha uwoga cha kigaidi kilichowalenga raia wasio na hatia."

Gavana wa New York Andrew Cuomo ameeleza shambulio hilo limetekelezwa na mtu mpweke, akisema hakuna ushahidi unaoonesha lilikua sehemu ya mpango mkubwa zaidi.

Tukio hilo lilitokea katika njia ya wapita baiskeli na watu wanaotembea kwa miguu karibu na eneo la makumbusho ya World Trade Center kusini mwa kisiwa cha Manhattan, kulikotokea mashambulio ya kigaidi ya Septemba 11, 2001.

Kamishna wa polisi wa New York James O'Neill amasema ilikua karibu saa tisa za mjioni wakati dereva akiwa na lori dogo alipopita katika njia hiyo ya kupita baiskeli, akiwagonga watu wanaopita. .

Polisi wanamueleza dereva huyo Sayfullo Saipov ni mhamiaji mzaliwa wa Uzbekistan, mwenye umri wa miaka 29 mweney makazi yake katika jimbo la Florida.

Mshambulizi wa New York Sayfullo Saipov.

Rais Donald Trump katika ujumbe kwenye ukurasa wake wa twitter aliandikja, "Haijabidi kuruhusu ISIS kurudi, au kuingia nchini kwetu baada ya kuwashinda huko Mashariki ya Kati na kwengineko. Imetosha."

Wizara ya usalama wa ndani imeimarisha usalama katika jiji la New York na kuruhusu gwaride la kuadhimisha Haloween kuendelea kwa kusema Marekani haitotishwa na magaidi.