Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 18:08

Rais Obama kukutana na Jenerali McCrystal leo.


Rais Barack Obama ataamua iwapo amfute kazi kamanda wake huko Afghanistan baada ya afisa huyo wa kijeshi Jenerali Stanley McCrystal, na baadhi ya washauri wake kutowa taarifa za kumdharau rais na maafisa wengine wakuu wa utawala wa Obama.

Rais Obama alichukuwa hatua isiyo ya kawaida ya kumuamrisha jenerali McCrystal kurejea nyumbani kwa mkutano hapo Oval Office hii leo, baada ya kusoma taarifa ambayo msemaji wa white house Robert Gibbs anasema yalimkasirisha rais.

“Kiwango na uzito wa kosa hili ni kubwa sana.” Alisema Gibbs.

Gibbs alisema kosa lilikuwa ni kusema mambo na kukubali washauri wake kusema mambo ambayo yanapuuza kipaumbele cha timu ya usalama wa taifa iloteuliwa na rais Obama, nayo ni kuwashinda Taliban na makundi kama hayo huko Aghanistan, ili wanajeshi wa Marekani waweze kuanza kurejea nyumbani mwaka ujao.

Gibbs alisema, chocohote chaweza kutokea katika kuamua hatma ya jenerali McCrystal .

Katika ripoti ya jarida la Rolling Stone, McCrystal ananukuliwa akipuuzilia umuhimu wa mkutano alofanya awali na rais Obama,kumkejeli makamu rais Biden na kumshutumu balozi wa Marekani huko Afghanistan Karl Eikenberry, kwa kumsaliti katika ugomvi juu ya sera. Kulingana na ripoti hiyo, McCrystal hukusema lolote pale washauri wake walimpomkejeli makamu rais , mshauri wa usalama wa taifa jenerali mstaafu James Jones, na mjumbe maalum wa Marekani kwa Afghanistan na Pakistan, balozi Richard Holbrooke.

Hiyo jana jenerali McCrystal aliomba msamaha kwa ripoti hiyo akiita kosa la kutotumia busara. Alisema anaheshima kubwa kwa rais, na timu yake ya usalama wa taifa. Aliwapigia simu baadhi yao hiyo jana.

Waziri wa ulinzi wa Marekani Robert Gates alimpendekeza McCrystal kupewa wadhifa wa kuongoza wanajeshi huko Afghanistan mwaka mmoja ulopita, na kumfuta kazi jenerali alokuwepo awali. Tangu wakati huo na mara kwa mara tangu hapo, Gates amemwita McCrystal mtu anayefaa kwa kazi hiyo, na kusema ana ufahamu mzuri wa jinsi ya kushughulikia suala la kupigana dhidi ya waasi, ambalo Afghanistan inahitaji.

Bw Gibbs alisema uwamuzi wa rais Obama utatangazwa hii leo jumatano, baada ya mkutano wa faragha huko White House na jenerali McCrystal na mkutano ulopangwa awali na timu yake ya usalama wa taifa kujadili hali ya Afghanistan.

XS
SM
MD
LG