Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 03:54

Marekani yalaani mauaji wa Padri Mushi


Askofu Mkuu wa Tanzania Kardinali Pengo azungumzia kifo cha Mushi
please wait

No media source currently available

0:00 0:00:38 0:00

Tukio la kuuawa kwa kupigwa risasi padre wa kanisa Katoliki visiwani Zanzibar Jumapili na matukio mengine ya mauaji na vurugu zinazohusiana na dini, vimeelezwa kwamba vinaweka reheni amani na usalama wa nchi hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam leo juu ya mauaji ya Paroko wa Kanisa Katoliki Minara Miwili Zanzibar, Evarist Mushi , Askofu Mkuu wa jimbo kuu katoliki la Dar es salaam, Polycarp Kardinali Pengo, amesema "mauaji hayo si pigo kwa kanisa Katoliki pekee bali ni pigo kwa mustakabali wa amani ya Tanzania wakati huu ambapo inashuhudiwa mauaji ya kihusisha imani za kidini."

Akikumbusha pia tukio la kunusurika kuuwawa kwa padre mwingine wa kanisa katoliki aliyepigwa risasi visiwani humo hivi karibuni.

Ripoti ya Dinah Chahali
please wait

No media source currently available

0:00 0:02:33 0:00
Kiungo cha moja kwa moja

Hata hivyo Polycarp Kardinali Pengo alitupia lawama vyombo vya ulinzi na usalama huko Tanzania, kutokana na kile alichodai kushindwa kudhibiti vitendo vya kihalifu na mauaji vinavyochochewa kwa misingi ya kidini.

Kwa upande wake Mkuu wa jeshi la polisi nchini IGP Said Mwema amewataka watanzania kuwa na subra wakatio huu ambapo timu maalum ya jeshi hilo imetumwa visiwani zanzibar kushughulikia tukio hilo la mauaji.

Rais Jakaya kikwete naye kupitia kurugenzi ya mawasiliano Ikulu ameagiza kuwepo uchunguzi wa haraka wa tukio hilo la mauaji ya paroko wa kanisa Katoliki. Padre aliyeuawa Evarist Mushi, anatarajiwa kuzikwa siku ya Jumatano Febuari 20 , katika makaburi ya Kitope yaliyopo nje ya mji wa Zanzibar.

Wiki iliyopita vurugu za kidini huko Geita pia zilisababisha mauaji ya Mchungaji Mathayo Kachila wa Kanisa la Tanzania Assemblies Of God katika mgogoro wa kuchinja nyama.

Wakati huo, huo Marekani imelaani vikali mauaji yasiyo na msingi ya Padre Evaristus Mushi wa Zanzibar. Taarifa iliyotolewa na ubalozi wa Marekani nchini Tanzania inasema mauaji hayo ya kikatili ni ya tatu kufanyika na kulenga viongozi wa kidini visiwani Zanzibar tangu Novemba mwaka jana ambayo yanakiuka pia thamani, utamaduni na amani ya Zanzibar, kisiwa kinachojulikana kwa utajiri wa kitamaduni, kustahamiliana.

Taarifa hiyo ilieleza kwamba Ghasia za kidini hazina nafasi Tanzania au kwingineko. Marekani inasimama kama mshirika mkuu wa raia wote wa nchi hiyo na inatoa wito kwao kuendelea kupinga ghasia zinazofanywa na wale wanaotaka kuhujumu usalama wa raia wenzao.
XS
SM
MD
LG