Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Julai 27, 2024 Local time: 04:18

Mgogoro wa bajeti ya Marekani ni matokeo ya miaka mingi ya mivutano ya kisiasa


Alama za kufungwa kwa baadhi ya shughuli za serikali zinaonekana pia hata kwenye Statue of Liberty huko New York, October 1, 2013.
Alama za kufungwa kwa baadhi ya shughuli za serikali zinaonekana pia hata kwenye Statue of Liberty huko New York, October 1, 2013.
Kuendelea kufungwa kwa baadhi ya shughuli za serikali ya Marekani ni matokeo ya miaka kadha ya tofauti za kisiasa nchini humu zinazotokana na mvutano baina ya vyama viwili vikuu vya siasa vya Demokratik na Republican kuhusu wajibu wa serikali kuu katika maisha ya wamarekani. Chimbuko la mgogoro huo lilianza karibu miaka 20 iliyopita na kuongezeka katika miaka ya 1990 kufuatia kuchaguliwa kwa Bill Clinton kama rais.

Warepublican walishindi udhibiti wa mabaraza yote ya bunge mwaka 1994 kwa mara ya kwanza katika muda wa miaka 40. Tofauti katika matumizi na wajibu wa serikali yalisababisha shughuli za serikali kufungwa mara mbili. Uchaguzi uliofuata wa mwaka 2000 ambao ulikuwa na upinzani mkali na kuishia kwa George W. Bush kuchaguliwa kuwa rais pia uliongeza hali ya siasa za kichama.

Mchambuzi Larry Sabato wa chuo kikuu cha Virginia anasema ongezeko la siasa za kichama lilitokea wakati wa awamu ya pili ya utawala wa Rais Bush. “Hakuna shaka kwamba tofuati ziliongezeka kwanza katika utawala wa Bush kwa sababu ya vita vya Iraq na alivyoshughulikia janga la Katrina. Na kuongezeka zaidi alipochaguliwa Rais Obama.”

Tofauti hizo zilizidi kupanuka Rais Obama aliposhinikiza mageuzi yake ya huduma za afya katika bunge mwaka 2010 bila hata kura moja ya Mrepublican. Hilo lilichochea makundi ya wakonsevativu wa Tea Party kote nchini, kundi lenye nguvu katika chama cha Republican.

Mgogoro wa kisiasa
Mgogoro wa kisiasa


Sheria ya huduma za afya, inayojulikana pia kama Obamacare, ndio kiini cha mgogoro uliosababisha kufungwa kwa shughuli za serikali baina ya Ikulu na bunge. Warepublican wamefanya juhudi kadhaa kuondoa fedha katika mpango huo wa afya au kuchelewesha utekelezaji wake.

Rais Obama anaamini sheria hiyo ni kioo cha machafanikio ya urais wake, na kwa kuungwa mkono na wabunge wademokrat anapinga jaribio lolote la kuizuia au kuichelewesha.

Kinachobishaniwa katika sheria hiyo ya Obamacare ni kile kinachoonekana kama wajibu wa serikali, anasema mtafiti wa chuo Quinnipiac Peter Brown. “Warepublican wanapenda serikali ndogo na matumizi madogo serikalini kwa hiyo wanapinga Obamacare. Wademokract wanaounga mkono kuhusika kwa serikali katika maswala mengi ya jamii na wanaona Obamacare kama kitu kizuri kufanya katika swala la afya.”

Upinzani dhidi ya sheria ya afya unaoongozwa na kundi la warepublican wakonsevativu katika baraza la wawakilishi, wengi wao wakiwa wanatumaini ungwaji mkono na wanaharakati wa Tea Party katika kuchaguliwa kwao.

Mchambuzi Larry Sabato anasema wengi wao wako tayari, angalau kwa sasa, kukubali lawama ya kulazimisha kufungwa kwa Shughuli za serikali. “Kutakuwa na gharama kubwa watakayolipa lakini inaelekea wako tayari kwa hilo kwa sababu wengi wao wako salama katika wilaya zao za uchaguzi. Kitu ambacho kinaweza kuwatia Wasiwasi ni changamoto wanayoweza kupata kwa warepublican wa mrengo wa kulia wakati wa uchaguzi wa awali.”

Kwa sasa, Larry Sabato haoni ufumbuzi wowote wa haraka kuhusu kufungwa kwa shughuli za serikali hali ambayo inaongeza sintofahamu kwa sababu bunge karibuni litalazimika kuongeza kiwango cha kukopa ili kuepuka serikali ya Marekani kushindwa kulipa madeni yake.

Mara ya mwisho serikali ilifunga shughuli zake Disemba 1995 na hali hiyo iliendelea kwa wiki tatu. Wachambuzi wanasema hatua hiyo ndio ilimsaidia Rais Bill Clinton kushinda awamu ya pili madarakani mwaka 1996.
XS
SM
MD
LG