Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 04:54

ICC yaanza tena kusikiliza kesi ya Ruto


Naibu Rais wa Kenya, William Ruto akiwa katika chumba cha mahakama ya ICC huko The Hague
Naibu Rais wa Kenya, William Ruto akiwa katika chumba cha mahakama ya ICC huko The Hague
Mahakama ya kimataifa ya uhalifu-ICC inaendelea kusikiliza kesi ya Naibu Rais wa Kenya, William Ruto baada ya kumruhusu arudi nyumbani kwa muda kukabiliana na shambulizi la wanamgambo wa al-Shabab lililosababisha vifo kwenye jengo la maduka ya kifahari la Westgate mjini Nairobi.

Ruto alirudi tena katika mahakama ya The Hague Jumatano kwa mashtaka juu ya uhalifu dhidi ya binadamu. Kesi yake ilianza mwezi uliopita huku waendesha mashtaka wakimshutumu kupanga ghasia za kikabila baada ya uchaguzi mkuu wa urais nchini Kenya uliokuwa na utata mwaka 2007. Wote washtakiwa Ruto na mwandishi wa habari Joshua Sang wanakana mashtaka.



Pia Jumatano mahakama ilitoa waranti ya kukamatwa kwa raia mmoja wa Kenya aliyeshutumiwa kwa kujaribu kuwahonga mashahidi waliohusika katika kesi za ICC kuhusiana na maafisa wa Kenya. Waendesha mashtaka wanasema Walter Osapiri Barasa alipendekeza kuwalipa mashahidi ili wasitoe ushahidi katika kesi hiyo na kwamba kukamatwa kwake ni muhimu ili kuhakikisha hakwamishi kuendelea kwa kesi hiyo.

Mwendesha mashtaka mkuu wa ICC, Fatou Bensouda anasema mahakama inatarajia maafisa wa Kenya watamkamata Barasa na kumpeleka kumweka kizuizini.

Barasa aliviambia vyombo vya habari Jumatano kwamba shutuma zinazotolewa dhidi yake ni za uongo.

Shirika la habari la Uingereza-Reuters linamkariri mwanasheria mkuu wa Kenya akisema waranti iliyotolewa na ICC ni utaratibu wa kimahakama kabla ya Kenya kuchukua utaratibu kama huo.

ICC pia imepanga mwezi Novemba kuanza kusikiliza kesi ya Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta juu ya mashtaka yanayohusiana na ghasia za baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2007.
XS
SM
MD
LG