Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 17:02

Wanaharakati walaumu watu kujichukulia sheria mkononi Congo.


Waasi wa kundi la M23 wakibeba bidhaa karibu na mpaka wa Congo na Uganda huko Bunagana, DRC.
Waasi wa kundi la M23 wakibeba bidhaa karibu na mpaka wa Congo na Uganda huko Bunagana, DRC.
Huko jamhuri ya kidemokrasi ya Congo , wanaharakati wa makundi ya kijamii wanasema magenge yameua watu 9 wanaotuhumiwa kwa uhalifu katika mji wa mashariki wa Goma tangu mwezi Novemba. Wanaharakati hao wanalaumu ongezeko kwa kile kinachoitwa watu kujichukulia sheria mkononi kwa vile serikali imeshindwa kuwasaka na kuwafunga zaidi ya wafungwa elfu moja mia moja waliokimbia jela.
Mauaji holela si kitu cha ajabu huko Goma, hata kabla ya kundi la waasi la M23 kuchukuwa udhibiti wa mji huo mwezi Novemba, na baadae kuondoka mapema mwezi Desemba. Lakini tangu hapo viongozi wa makundi ya kiraia na wa serikali, wanasema kumekuwepo na ongezeko la idadi ya washukiwa wahalifu kuuwawa na magenge.
Jean Pascal Mugaruka ni kaimu mkuu wa kundi la kiraia kwa mji wa Goma
anaiambia sauti ya America kuwa tangu mwishoni mwa Novemba, takriban watu 9 wamechomwa moto wakiwa hai, kwa sababu walipatikana wakiiba au waligundulika wakidhibiti mali iliyoibiwa.
Kwa mujibu wa Mugaruka, watu wamekuwa wakichukuwa sheria mikononi mwao kwa sababu mfumo wa sheria haufanyi kazi ipasavyo na wamekereka kuwa zaidi ya wafungwa elfu moja mia moja waliachiliwa kutoka jela.
Pia watu wamekuwa wakilipiza kisasi kwa unyanyasaji waliofanyiwa na waasi wa M23.
Vyanzo kadhaa vimeiambia sauti ya America kwamba wafungwa katika jela kuu, waliachiliwa na wanajeshi hapo Novemba 20, kabla jeshi la Congo kuondoka Goma na kuwaachia waasi.
Karibu mwezi mzima wa Desemba, jela hiyo ili haitumiki, lakini katika wiki mbili zilizopita, baadhi ya majengo yamefunguliwa tena.
Anasema sasa jela inafanya kazi tena mjini Goma, kwa hivyo watu kujichukulia sheria mikononi hakutastahmiliwa tena, ingawaje mfumo wa sheria haufanyi kazi vilivyo, na mahakama za kijeshi bado hazijaanza tena kufanya shughuli zake.
Anasema makundi ya kiraia yamezungumza dhidi ya mauaji holela na yanapanga harakati za kuwaelimisha watu dhidi ya vitendo hivyo.
Makundi ya kiraia mjini Goma yanaitaka serikali kuwasaka wafungwa waliotoroka, wengi wao ambao ni wanajeshi waliopatikana na hatia ya wizi wa kutumia silaha.
Mugaruka anasema hadi sasa chini ya wafungwa 20, wamerudishwa kwenye jela kuu, lakini serikali bado inaendelea kuwasaka wengine.
Anasema jeshi la polisi limeahidi tuzo ya dola mia moja kwa mtu yeyote atakayetowa maelezo yatakayopelekea kukamatwa kwa mfungwa aliyetoroka, na kwamba serikali pia wameandaa doria mchanganyiko za jeshi na polisi ambao wanawafuatilia majambazi, na majambazi wengine wameuwawa.
XS
SM
MD
LG