Uchaguzi mkuu Marekani: Bunge labaki vile vile

Jengo la Bunge la Marekani, Washington DC

Uchaguzi mkuu Marekani umemalizika huku kukiwa na mabadiliko kiasi ya viti vya bunge, uwiano wa madaraka kati ya baraza la Seneti na bunge unabaki kuwa vile vile.

Katika baraza la seneti chama cha Democrat kimeongeza angalau kiti kimoja na chama cha Republican kimepoteza kiti kimoja, hii ikimaanisha kuwa baraza la seneti mwaka 2013 litakuwa na wademocrat wasiopungua 51, wa-Republicans wasiopungua 44 na angalau viti viwili vya wabunge wa kujitegemea. Viti vitatu bado havijajulikana vitakuwa vinaegemea chama gani.

Akizungumza na Sauti ya Amerika, Professa Julius Nyang’oro wa chuko kikuu cha North Carolina alisema Wademocrat wamepiga hatua kubwa katika baraza la seneti ambapo jimbo la Massachusetts, m-Democrat Elizabeth Warren alimshinda Seneta wa sasa Scott Brown kutoka chama cha Republican. Chama cha Democrat kimechukua ushindi pia katika jimbo la Virginia lenye upinzani mkali, ambapo gavana wa zamani wa Democrat Tim Kaine alimshinda gavana wa zamani wa Republican, George Allen.

Your browser doesn’t support HTML5

Mhadhiri Julius Nyang'oro, North carolina, Marekani


Chama cha Democrat pia kimepata ushindi katika jimbo la Indiana ambapo mwakilishi wake Joe Donnelly alimshinda m-Republican Richard Mourdock. Mpambano huo umeonyesha mwamko wa kitaifa baada ya Mourdock kutoa matamshi yenye utata kuhusu ubakaji na utoaji mimba.

Kukiwa na viti 15 kati ya 435 ambavyo bado havijulikani, ishara pia zinaonyesha kutakuwa na mabadiliko kiasi katika bunge. Wa-Republican hivi sasa wana viti 233, wakati wa-Democrat wameshinda viti 187. Spika wa bunge, mrepubliban John Boehner kutoka jimbo la Ohio inaonekana ataendelea kushikilia nafasi yake ya kuongoza bunge. Katika taarifa ya Jumanne usiku, Boehner alisema wa-republican wataendelea kupinga wito wowote wa kuongeza kodi. Lakini pia alisema kuwa tayari kushirikiana na yeyote atakayeshinda uchaguzi wa rais.