Rwanda haiwezi kuzungumza na FDLR

Marais wa Rwanda Paul Kagame, Jakaya Kikwete wa Tanzania, Yoweri Museveni wa Uganda na Joseph Kabila wa Congo mjini Kampala Ogusti 7 2012

Rwanda haiwezi kuzungumza na watu wanaotuhumiwa kuwauwa takriban watu milioni moja na wenye mpango wa kuendelea na mpango wao wa mauwaji, amesema Balozi wa Rwanda mjini Washington James Kimonyo.

Akizungumza na Sauti ya Amerika kufuatia wito wa rais Jakaya Kikwete kwa marais wa mataifa ya maziwa Makuu marais Paul Kagame, wa Rwanda, Joseph Kabila wa jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Yoweri Museveni wa Uganda, kuzungumza na makundi ya waasi wanapambana na nchi zao.

Your browser doesn’t support HTML5

Mahojiano na Balozi Kimonyo


Balozi Kimonyo anasema ni lazima kutofautisha kati ya mazungumzo na makundi ya upinzani dhidi ya serikali na kundi la uwasi lililosababisha mauwaji ya halaiki kama FDLR.

Anasisitiza kwamba serikali ya Rwanda na washirika wake kwa msaada wa Umoja wa Mataifa na Benki Kuu ya Dunia wameweka mpango wa kuwaruhusu Wanyarwanda wanaoishi huko DRC wanaotaka kurudi nyumbani kuweza kufanya hivyo na wanapatiwa makazi na hata kuweza kuandikishwa katika jeshi au kupatiwa kazi nyingine.

Wakati huo huo kundi la wanusurika wa mauaji ya maangamizi ya Rwanda wanaoishi Marekani wamemwandikia barua rais Barack Obama wa Marekani kulalamika kuhusu matamshi ya rais Jakaya Kikwete wa Tanzania kuitaka Rwanda kuzungumza na waasi wa FDLR. Kundi hilo limemtaka Rais Obama aungane na wanusurika hao kumtaka rais Kikwete akanushe usemi wake wakati wa mkutano na viongozi wa Rwanda mjini Addis Ababa mwishoni mwa wiki.

Rais Kikwete alikaririwa na radio ya kimataifa ya Ufaransa -RFI- akitoa wito kwa Rwanda kuzungumza na FDLR, kundi ambalo linashutumiwa kwa kuendesha mauaji ya maangamizi ya mwaka 1994 na ambalo sasa linaendesha shughuli zake mashariki mwa Congo.

Wanusurika hao wamemtaka rais Kikwete aombe radhi hadharani kwa wanyarwanda , wacongo na watu wengine walioathirika na vitendo vya kundi la FDLR.