Israel yafanya mashambulizi ya anga dhidi ya Syria

Mji wa Damascus, Syria, ulioshambuliwa na Isreal. Picha ya maktaba

Shirika la habari la serikali ya Syria la SANA limesema Jumapili kwamba Israel imefanya mashambulizi ya anga kwenye mji mkuu  ambapo watu watano wamekufa huku wengine takriban 15 wakiachwa na majeraha.

Mashambulizi ya roketi yameripotiwa kupiga kitongoji cha Kafr Sousa, mjini Damascus, karibu na kituo cha usalama ambako majengo kadhaa ya makazi yameharibiwa.

Hakujakuwa na tamko lolote kutoka jeshi la Israel ambalo kwa kawaida halitoi ripoti kuhusu mashambulizi ya Syria. Maafisa wa Israel katika siku za nyuma wamesema kwamba jeshi lao huwa halilengi makazi ya watu wakati wote likijiepusha kufanya uharibifu kwenye maeneo hayo iwezekanavyo.

Chombo cha habari cha upinzani cha Syria cha Orient News kimedai kuwa shambulizi hilo lililenga maafisa wakuu wa kundi la wapiganaji wa Iran kwenye kituo maarufu kama Kafar Sousah.