Novemba 2022, serikali ya Ethiopia na viongozi kutoka eneo la Tigray walifikia makubaliano ya kusitisha mapigano, yanayojulikana kama Mkataba wa Pretoria, baada ya vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyodumu kwa miaka miwili vilivyoharibu sehemu kubwa ya kaskazini mwa Ethiopia.
Mike Hammer, mjumbe maalum wa Marekani katika Pembe ya Afrika, ameiambia VOA wakati wa mahojiano maalumu ya Jumatatu kwamba Ethiopia inasonga mbele katika mwelekeo sahihi. Alibainisha kuwa wakimbizi wa ndani wameanza kurejea makwao, na ukiukwaji wa haki za binadamu katika mkoa wa Tigray umepungua kwa kiasi kikubwa.
Lakini alikiri kuendelea kwa migogoro katika mikoa ya Amhara na Oromia, akisema kuwa Marekani iko tayari kuunga mkono juhudi zozote za kuleta amani katika maeneo hayo kwa njia ya mazungumzo.
Hammer alisafiri kwenda Ethiopia wiki iliyopita kuhudhuria mkutano wa pili wa Umoja wa Afrika wa kukagua utekelezaji wa Mkataba wa Pretoria.
Akielezea ahadi zilizowekwa na serikali ya Ethiopia na TPLF chini ya mkataba wa Pretoria, amesema kile alichokiona ni kwamba pande zote zimejikita katika kuhakikisha zinafuata makubaliano yaliyoafikiwa, na ndiyo sababu Marekani inaendelea kuwa karibu kutoa msaada wa juhudi zozote zile zinazofanikisha kufuatwa kwa makubaliano na kuepusha kurejea kwa ghasia.
Forum