Bunge la Tanzania Alhamisi limemthibitisha Kassim Majaliwa mwenye umri wa miaka 54 kama Waziri Mkuu mpya nchini humo kufuatia uteuzi wa Rais John Magufuli katika wadhifa huo.
Uteuzi wa Majaliwa haukutazamiwa na wengi ingawa ni mtu ambaye ameshika nafasi mbali mbali nchini ikiwa ni pamoja na waziri katika ofisi ya Waziri Mkuu katika serikali iliyopita ya Rais Jakaya Kikwete.
Maoni yaliyotolewa na baadhi ya wananchi, mara baada ya kutangazwa, yanaonyesha kuwa wameridhishwa na uteuzi huo ambao unaleta sura mpya katika siasa za Tanzania.
Wakati wa kampeni za uchaguzi mwaka huu kauli mbiu kubwa kwa chama tawala cha CCM na wapinzani kilikuwa mageuzi na wengi wanadhani huenda huu ni mwanzo wa mageuzi hayo katika siasa za nchi hiyo.