Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 16:11

Madakatari Tanzania watangaza mgomo usio na kikomo.


Wafanyakazi wa huduma katika hospitali ya Muhimbili wakipokea wagonjwa baada ya madaktari kugoma.
Wafanyakazi wa huduma katika hospitali ya Muhimbili wakipokea wagonjwa baada ya madaktari kugoma.

Mgomo wa madaktari nchini Tanzania umetangazwa wakati serikali imedai inashughulikia madai na kuwataka waendelee na kazi.

Madaktari nchini Tanzania Jumatano wametangaza mgomo usio na kikomo ili kuishinikiza serikali ya nchi hiyo kutimiza ahadi za kuboresha maslahi yao ikiwemo pia kuwawajibisha viongozi wakuu wa wizara ya afya.

Mgomo huo mpya unatokea siku moja baada ya serikali kuwaomba madaktari hao kuendelea na kazi wakati madai yao ya msingi yakiendelea kushughulikiwa.

Makamu wa rais wa chama cha madaktari Tanzania. MAT Dakta Primus Saidia amesema katika kikao chao kilichofanyika katika ukumbi wa Russia hadi mchana wa Jumatano, madaktari hao wameazimia kufanya mgomo usio na kikomo kushinikiza serikali kutatua madai yao.

Jijini Dar es salaam katika hospitali kadhaa zikiwemo za Muhimbili, mwananyamala na Amana hali ya upatikanaji wa huduma kwa wagonjwa haikuwa ya kuridhisha.

Hali kama hiyo imeripotiwa jijini Mwanza ambako Madaktari waliopo katika mafunzo ya vitendo katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando wametangaza kuanza mgomo ili kuungana na wenzao wakidai watahitimisha mgomo huo iwapo waziri wa Afya na naibu wake wataachia ngazi.

Afisa Uhusiano wa kitengo cha mifupa Muhimbili, Moi, Almasi Juma hata hivyo amesema kwamba kwa siku ya kwanza ya mgomo, hali ya upatikanaji wa huduma haikuwa mbaya sana licha ya kuonyesha wasiwasi kwa siku zijazo.

Wakati hayo yakiendela, Waziri Mkuu Mizengo Pinda amesema Serikali imejipanga kukabiliana na mgomo mwingine wa madaktari, ikiwa hawatakubali ushauri wa serikali juu ya kusitisha mgomo huo.

Madai mengine ya madaktari ni nyongeza ya posho ya wito wa dharura, posho za nyumba magari pamoja mazingira magumu ya kazi.

XS
SM
MD
LG