Jimbo la kusini-magharibi la Texas jana limeripoti kile kinachoonekana kuwa kesi ya kwanza ya kirusi cha ZIKA ambacho kimeambukizwa kwa mtu aliyeko Marekani kwa njia ya ngono.
Maafisa katika kaunti ya Dallas wanasema mgonjwa huyo aliambukizwa ZIKA baada ya kufanya mapenzi na mtu mgonjwa ambaye aliwasili hapa nchini kutoka eneo ambalo hivi sasa linakumbwa na kirusi hicho.
Kaunti hiyo baadaye iliripoti kwenye mtandao wa twitter kwamba mtu aliyeathiriwa hivi karibuni alisafiri kwenda Venezuela. Kitengo cha kudhibiti na kuzuia magonjwa hapa Marekani - CDC - kimethibitisha kesi ya ZIKA katika jimbo la Texas.
Shirika la afya Duniani lilitangaza Jumanne kwamba Zika imekua dharura ya afya ya umaa duniani, na hivyo mikakati inabidi kutayarishwa kupambana na ugonjwa huo.