Milio ya risasi imesikika nchini Burkina Faso karibu na kasri ya rais,baada ya mamia ya wandamanaji kuvamia majengo ya bunge na kuyaasha moto.
Mapema Alhamis hali ya tahadhari ilitokea wakati wabunge wakijiandaa kupiga kura juu ya mabadiliko ya katiba ambayo yatampa fursa Rais wa muda mrefu Blaise Compaore kugombania kuongoza kwa muhula mwingine.
Mwandishi wa Sauti ya Amerika aliyepo Ouagadougou, anasema polisi wa kuzima ghasia walitumia gesi ya kutoa machozi na maji, lakini walishindwa kuwazuia waandamanaji nje ya bunge, ambao waliweza kuvunja vizuizi na kuingia ndani ya jengo hilo.
Vilevile wameonekana askari wa kikosi cha kumlinda rais wakipiga risasi hewani katika juhudi za kuwazuia waandamanaji kuendelea kuelekea katika kasri ya rais, ambapo kijana mmoja alipigwa risasi kichwani.
Msemaji wa serikali ameiambia Sauti ya Amerika kuwa, mabadiliko hayo ya katiba yaliyowasilishwa yameondolewa, na televisheni ya taifa pia, imeripoti habari hiyo. Baadaye televisheni hiyo ilikaonekana kutokuwa hewani. Rais Compaore ameongoza Burkina Faso toka mwaka 1987.