Bunge la Jamhuri ya muungano wa Tanzania imepiga kura Jumanne kupitisha bajeti ya nchi hiyo ya kiasi cha shillingi trilioni 22.4, ikiwa ni ongezeko la trilioni 2 ukilinganisha na bajeti ya mwaka 2014/15.
Akizungumnza na Sauti ya Amerika juu ya bajeti hiyo , mwenyekiti wa chama cha upinzani cha CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, amesema bajeti ya nchi hiyo imekaa kisiasa zaidi kwasababu ni mwaka wa mwisho wa Rais Jakaya Kikwete na ataitekeleza kwa miezi minne tu.
Profesa Lipumba aliongeza kusema kwamba bajeti hiyo imepandisha bei ya mafuta ya petrol na taa, kwa madai kwamba fedha zitatumia katika miradi ya maendeleo vijijini. Lakini anasema, matokeo yake itaathiri bei ya usafiri na mambo mengine yote ikiwa ni pamoja na chakula.
Kwa upande wa mapato anasema kwamba mapato ya ndani ni madogo kuliko matumizi ya kawaida kwa hiyo bajeti ya maendeleo bado inaendelea kutegemea misaada kutoka nje.