Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 19:15

Muda ndio muhimu katika kutambua na kutibu ugonjwa wa Ebola-VOA.


Mtangazaji wa VOA wa kipindi cha "Straight Talk Africa" Shaka Ssali, akiwa na balozi Bockari K. Stevens wa Sierra Leone mjini Washington Dc, Dr. Malonga Miatudila, na mgonjwa aliyepona Ebola Rick Sacra na Ashoka Mukpo, Nov. 19
Mtangazaji wa VOA wa kipindi cha "Straight Talk Africa" Shaka Ssali, akiwa na balozi Bockari K. Stevens wa Sierra Leone mjini Washington Dc, Dr. Malonga Miatudila, na mgonjwa aliyepona Ebola Rick Sacra na Ashoka Mukpo, Nov. 19

Muda ndio jambo muhimu sana katika kutambua na kutibu wale walioambukizwa ugonjwa hatari wa Ebola. Huo ndio ujumbe wa mkutano maalum ulioandaliwa na Sauti ya Amerika (VOA) mjini Washington siku ya Jumatano na kutangazwa moja kwa moja na kipindi cha Straight Talk Africa.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo ni kwamba tangu kuripotiwa watu wa kwanza waloambukizwa na ugonjwa huo wa hatari mwezi Machi huko Afrika Magharibi, virusi hivi vya hatari vimeshawaathiri watu wapatao 14,500 huko Liberia, Sierra Leone na Guinea, na zaidi ya watu 5,400 wamefariki dunia .

Ingawa kumekuwa na kesi kadhaa za ugonjwa huo katika maeneo mengine duniani ikiwa ni pamoja na Marekani, nchi hizo tatu za Afrika zimebaki kuwa ndio kitovu cha ugonjwa huu.

Katika mkutano huo wa Straight Talk kipindi cha televisheni cha VOA wataalam kadhaa walijadili juu ya dharura ya kuwatambua na kuwatibu wagonjwa wa Ebola.

Dr.Malonga Miatudila alisaidia kutambua ugonjwa huo 1976. Katika muda miaka 40 iliyopita anasema kumekuwa na milipuko 25 , na hakuna iliyodumu zaidi ya miezi 3. Hatua madhubuti za haraka ziliwezesha kudhibiti milipuko hiyo na kwa jumla mwishoni mwa 2013, Ebola ilikuwa imeuwa chini ya watu 2000.

Mlipuko huu ndio ulio mkubwa zaidi. Safari hii, Miatudila anasema muda mrefu ulipita kabla ya jumuiya ya wataalam wa afya na washirika duniani kushughulikia mlipuko huo .

Dr. Miatudila anasema "ulipoanza huko Guinea tulisubiri , tukangojea na tukangojea sana . Tulipoteza muda. Tulikaa kwa zaidi ya siku 100 kabla ya kukubali kuwa kuna tatizo.”

Jumuiya ya kimataifa ilichukua hatua na majibu kwa mzozo huo wa afya sasa ni mazuri.

Dr.Rick Saycra pia alikuwa katika jopo hilo. Yeye ni raia wa tatu wa Marekani kupata ugonjwa wa Ebola wakati akifanya kazi Afrika. Alipogundua ana dalili za awali ,Sacra alipimwa mara moja na kurudishwa Marekani kwa matibabu . Kutokana na utalaam wa kisasa katika hospitali moja huko Nebraska , Sacra alipona na anasema anashukuru sana kwa majibu ya haraka.

Katika nchi ambazo Ebola inaendelea kusambaa na wajumbe katika mkutano huo wa Sauti ya Amerika walisema moja ya changamoto kubwa sana ni kuwashawishi jamaa na marafiki wa wale waliofariki kuacha mila na tabia za mazishi ambazo zinawaweka karibu sana na miiili ya marehemu na virusi.

Wasikilizaji na watazamaji wa VOA walikumbushwa jinsi Ebola inavyosambaa kwa kugusana na maji maji ya mwili ya wale waliofariki na ugonjwa huo na waliombwa kuwaachia watalaam wa huduma za afya kushughulika na miili hiyo na kutafuta matibabu haraka mara waonapo wanapata dalili za kwanza kabisa za ugonjwa huo.

XS
SM
MD
LG