Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 23:10

Ufaransa yaanza operesheni ya ardhini Mali


wanajeshi wa Ufaransa wakiwa Bamako nchini Mali
wanajeshi wa Ufaransa wakiwa Bamako nchini Mali
Majeshi ya Ufaransa yameanza operesheni ya nchi kavu nchini Mali kuelekea mji wa Niono ambao upo kusini ya eneo moja lililotekwa mwanzoni mwa wiki hii na wanamgambo wa ki-Islam ambao wanadhibiti eneo la kaskazini mwa nchi hiyo.

Waziri wa Ulinzi wa Ufaransa Jean-Yves Le Drian alisema mapigano nchini Mali yatakuwa ya muda mrefu na kwamba majeshi yake yanaondoka kutoka mji mkuu kuelekea eneo lililoshikiliwa na waasi.

β€œLeo majeshi ya ardhini yanasambazwa. Hadi hivi sasa, tulikuwa na majeshi kadhaa mjini Bamako kulinda watu, raia wa ulaya na mji. Hivi sasa majeshi ya Ufaransa yanaelekea upande wa kaskazini.”

Mwandishi wa Sauti ya Amerika-VOA alisema msururu wa vifaru uliondoka Bamako Jumanne kuelekea kaskazini.

Ufaransa ilipeleka majeshi mara ya kwanza nchini Mali siku ya Ijumaa kufuatia ombi la serikali ya muda nchini humo na pia Ufaransa imeendelea kuingiza vifaa na wanajeshi ambao watafikia idadi ya 2,500. Serikali inasema majeshi yataendelea kuwepo hadi hali nchini Mali iimarike.

Nigeria inatarajia kupeleka wanajeshi 190 nchini Mali Jumatano, sehemu ya ahadi ya hiyo kuchangia wanajeshi 3,300 kwa jeshi la Afrika magharibi lililoidhinishwa na Umoja wa mataifa ili kusaidia kupambana na wanamgambo wa ki-Islam.

Wakati huo huo waziri wa ulinzi wa Marekani Leon Panetta alisema Jumanne kuwa Marekani inaunga mkono juhudi za Ufaransa nchini Mali lakini Marekani haitapeleka wanajeshi wake huko.
​
XS
SM
MD
LG