Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 18:32

Watanzania watoa ushahidi katika kesi ya Ghailani.


Kesi ya mtuhumiwa wa ugaidi ikiendelea huko New York.
Kesi ya mtuhumiwa wa ugaidi ikiendelea huko New York.

Mashahidi kadha wa mlipuko wa bomu katika ubalozi wa Marekani, Dar es Salaam mwaka 1998 watoa ushahidi katika kesi ya mtuhumiwa Ahmed Khalfani Ghailani mjini New York.

Waendesha mashitaka wa Marekani Jumatano waliendelea kuweka msingi wa kesi yao dhidi ya Mtanzania Ahmed Ghailani katika kesi ya kwanza kufanyika katika mahakama ya kiraia kwa mtuhimiwa wa ugaidi aliyekuwa akishikiliwa katika gereza la Guantanamo Bay, Cuba. Ghailani anakabiliwa na mashitaka ya kula njama katika ulipuaji wa balozi za Marekani, Dar es Salaam na Nairobi, Kenya mwaka 1998. Milipuko hiyo iliuwa watu 224, ikiwa ni pamoja na Wamarekani 12.

Ushahidi wa Jumanne ulitolewa na Watanzania wawili waliokuwa walinzi katika eneo la ubalozi wa Marekani mjini Dar es Salaam, pamoja na mwanamke mmoja ambaye alikuwa msaidizi wa kisiasa katika ubalozi, na mlinzi mmoja wa jeshi la Marine la Marekani.

Valentine Mathew Katunda, mmoja wa walinzi wa Kitanzania alitoa ushahidi kuwa mnamo August 7, 1998, alikuwa katika lindo nje ya ubalozi aliposikia mlio mkubwa kama radi. Akitoa ushahidi kwa Kiswahili kupitia mfasiri, Katunda alisema alijikuta ametupwa sakafuni kutokana na mlipuko huo na kupoteza fahamu. Alipozinduka alijikuta katika kifusi ambapo alibanwa kwa muda wa saa nne nzima.

Naye Justina Mdobilu, mwanasheria wa Tanzania ambaye alikuwa akifanya kazi katika ubalozi kama msaidizi wa maswala ya kisiasa na mfasiri, alieleza mahakama kuwa alikuwa akihudhuria mkutano na naibu balozi alipoona mlipuko nje kupitia dirishani. Alisema dirisha lilivunjikia ndani ya chumba na alichosikia “ilikuwa kishindo kikubwa kuliko vyote nilivyopata kusikia katika maisha yangu, maumivu makali yalipita kifuani kwangu hadi mgongoni.” Mdobilu ambaye alikuwa na mimba ya miezi minane wakati huo alikatika sehemu kadha na kutokwa damu lakini aliweza kutoka katika jengo la ubalozi huo. Mtoto wake alizaliwa bila madhara.

XS
SM
MD
LG