Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 13:30

Walonusurika ajali ya Nakuru wasimulia ‘safari yenye nuksi’


Rais Uhuru Kenyatta
Rais Uhuru Kenyatta

Maelezo zaidi juu ya ajali ya Jumamosi nchini Kenya iliyouwa watu 19 katika eneo la Soysambu kwenye bara kuu ya Nakuru-Nairobi yanadhihirisha kuwa tatizo lilianza mwanzo wa safari hiyo.

Dereva wa basi lenye viti 52 -FlashLink, linalomilikiwa na Super Highway Sacco, alichaguliwa kwa kubahatisha katika kituo cha basi cha Machakos kufuatia mabishano makali kati ya madereva.

Madereva hao walikuwa hawajakubaliana ni nani kati yao aendeshe basi katika safari hiyo, waliosalimika katika ajali hiyo wameeleza.

Safari hiyo ilichelewa kwa zaidi ya saa moja kufuatia mabishano hayo juu ya dereva gani awe nahodha wa chombo hicho.

Kwa mujibu wa taarifa ya Serikali ya Kenya, rais ameamrisha uchunguzi ufanyike mara mmoja kufuatia ajali hiyo.

Rais Uhuru Kenyatta ameagiza kuwa vyombo husika vianze uchunguzi kutafuta sababu ya chanzo cha ajali hiyo na kuchukua hatua zaidi kuhakikisha usalama wa barabara hizo wakati wote.

Ajali hiyo ambayo ilitokea eneo la Mbaruk, katika kaunti ndogo ya Gilgil ilihusisha magari matatu- basi lilouwa watu na malori mawili.

Watu kumi na nane walipoteza maisha papo hapo na mwengine alifia hospitali ya St Mary’s Mission Hospital akiuguza majeraha na wengine kumi na nne walijeruhiwa na saba kati yao walikuwa mahututi.

“Mtu mmoja kati ya kumi na nne waliokuwa wamelazwa amekufa lakini madaktari wetu waliweza kuwaokoa wale wengine waliojeruhiwa na sasa wako katika hali inayoridhisha,” Shadrack Musau, Muuguzi wa zamu katika Hospitali hiyo ya St Mary amesema.

Vyanzo vya habari nchini Kenya vimesema kuwa abiria waliosalimika wameeleza kuwa dereva wao alikuwa akiendesha kwa hatari na alionekana kutokuwa na uzoefu na bara hiyo.

Abiria mmoja aliyenusurika, Robert Otieno amesema kuliambia gazeti la Sunday Nation kuwa safari yao ilikuwa na mkosi tangu mwanzo walipopanda basi, inayotoa huduma katika njia 44 za Githurai katika eneo la Nairobi.

Baadhi ya abiria walidanganywa na hata kulazimishwa kupanda basi hilo, ambalo lilianza safari yake saa tano usiku.

Watu waliosalimika katika ajali hiyo wameliambia gazeti la Sunday Nation kuwa baadhi ya abiria walikuwa wametishia kushuka kutoka katika basi hilo wakati madereva hao walipokuwa wakibishana.

“Tulikuwa tumetishia kuwa tutavunja safari yetu kabla ya madereva hao kumchagua dereva kwa kubahatisha katika kituo kuendesha gari hilo mpaka Busia,” Mr Otieno amesema.

XS
SM
MD
LG