Waasi walio waaminifu kwa aliyekuwa makamu wa rais wa Sudan kusini Riek Machar, wamesifu makubaliano ya kushirikiana madaraka na serikali ya rais Salva Kiir, yaliyofanyika jana Alhamisi.
Wamesema azimio hilo ni muhimu na kwamba ni hatua mwafaka katika jitihada za kutafuta amani nchini humo. Makubaliano hayo yaliyotiwa saini mjini Juba, yanaipa serikali ya Salva Kiir nafasi 16 kwenye baraza la mawaziri, ikiwa ni pamoja na wizara za fedha na mipango, ulinzi, habari, usalama wa taifa na wizara ya sheria na maswala ya katiba.
Waasi wanaoongozwa na Machar wamepata nafasi 10, ikiwa ni pamoja wizara za mafuta, mambo ya ndani, kazi, madini na wizara ya ardhi, nyumba na maendeleo ya mjini.
Kundi la waliokuwa wafungwa wa kisiasa lisiloegemea upande wowote kisiasa, lilipewa wizara za Mambo ya nje na Uchukuzi, huku vyama vingine vya kisiasa nchini humo vikipewa nafasi mbili kwenye baraza hilo. Ezekiel Gatkuoth, ambaye ni katibu anayehusika na mambo ya nje katika kundi la chama cha Sudan People’s Liberation Movement (SPLM) lililoingia upinzani, amesema waasi watazingatia maafikiano hayo, ingawaje matakwa yao yote hayakutimizwa.