Vikosi vya Iraq vinavyoungwa mkono na wapiganaji wa Kikurdi wa Peshmerga wameanza kile wanachoeleza kuwa hatua ya kwanza ya kumaliza ngome ya kundi la Islamic State mjini Mosul.
Mapema leo, vikosi hivyo viwili vya Iraq vilivyopata mafunzo kutoka Marekani vimeanza mapigano dhidi ya vijiji 6 vilivyoshikiliwa na Islamic State kusini mashariki mwa Mosul.
Waliohusika pia ni makabila ya Sunni ambayo makamanda wa Peshmerga wamesema ni muhimu katika kushikilia maeneo asili ya Kisunni. Generali Najat Ali kutoka kikosi cha Kikurdi cha Peshmerga amesema kuwa vikosi vyake havihusiki moja kwa moja kwenye mashambulizi hayo yanayofanyika kwenye maeneo ya asili ya waarabu wa Kisunni lakini vinatoa ushauri wa kijasusi kwa vikosi vya Iraq kuhusu vijiji hivyo.