Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 14:20

Ubalozi wa Marekani Burundi unamhimiza Nkurunziza kutowania tena madaraka


Rais wa Burundi, Pierre Nkurunziza
Rais wa Burundi, Pierre Nkurunziza

Ubalozi wa Marekani nchini Burundi ulieleza kwamba unaendelea kumhimiza Rais Pierre Nkurunziza kuacha juhudi zake za kuwania muhula wa tatu, uamuzi ambao umezusha maandamano ya ghasia tangu rais kutangaza hivyo hapo April.

Ubalozi wa Marekani mjini Bujumbura unasema mpango wa bwana Nkurunziza unakiuka mkataba wa Arusha ambao ulimaliza miaka ya ghasia huko Burundi na unaweza kuhatarisha uthabiti ulopatikana baada ya juhudi kubwa kufuatia vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Ghasia za kisiasa Bujumbura
Ghasia za kisiasa Bujumbura

Taarifa ya ubalozi inaeleza kwamba hali ilivyo hivi sasa huko Burundi si muafaka kuweza kufanyika kwa uchaguzi ulio huru, haki, uwazi na wa kuaminika.Na hii inatokana na kufungwa nafasi za kisiasa, kufungwa kwa vyombo binafsi vya habari, na jinsi serikali inavyojibu kwa kutumia nguvu malalamiko ya kisiasa na kuendelea kwa ripoti za ghasia na ukandamizaji unaofanywa na wanamgambo vijana wenye silaha.

Rais alisema kupitia msemaji wake hapo Jumatatu kwamba atafikiria ombi hilo. Lakini naibu msemaji wa rais Gervais Abayeho aliiambia Sauti ya Amerika-VOA kwamba uchelewesha usisukume uchaguzi kwa muda mrefu sana.

Rais Nkurunziza alisema ana haki ya kuwania muhula wa tatu madarakani kwa sababu aliteuliwa kuongoza katika muhula wake wa kwanza na wala hakuchaguliwa na wananchi. Lakini wakosoaji wake wanasema muhula wa tatu utakuwa kinyume na katiba ya nchi.

Wakimbizi watoto katika kambi ya Rwanda
Wakimbizi watoto katika kambi ya Rwanda

Wakati huo huo, Umoja wa Mataifa ulieleza kwamba unatoa msaada wa dola milioni 15 kwa Rwanda na Tanzania ili kuzisaidia nchi hizo kukabiliana na mmiminiko wa wakimbizi kutoka Burundi. Umoja wa Mataifa unaeleza kwamba, asilimia 60 kati ya wakimbizi 70,000 ni watoto ambao wameukimbia mji mkuu wa Burundi, Bujumbura tangu ghasia za maandamano zilipoanza mwezi April.

Umoja wa Mataifa ulieleza watoto kutoka Burundi wamekuwa wakiwasili nchini Rwanda na Tanzania wakiwa wagonjwa na wenye utapiamlo. Inasema mlipuko wa kipindupindu uliathiri watu wapatao 4,000 katika miji iliyopo kwenye bandari ya ziwa Tanganyika na ugonjwa wenyewe uliuwa wakimbizi 30 katika kambi moja huko.

XS
SM
MD
LG