Tume ya Taifa ya Uchaguzi ya Tanzania, Ijumaa ilimkabidhi rasmi cheti cha ushindi wa urais wa Tanzania, kwa aliyekuwa mgombea wa Chama Cha Mapinduzi-CCM, Dr John Pombe Magufuli na mgombea mwenza wake bi, Samia Hassan Suluhu ambaye anakuwa mwanamke wa kwanza kushika wadhifa huo kwa upande wa Tanzania .
Hata hivyo chama kikuu cha upinzani cha CHADEMA na UKAWA pamoja na mgombea wake bwana Edward Lowassa hawakuhudhuria Hafla hiyo. Alhamisi mgombea urais kupitia muungano huo wa UKAWA aliwasilisha waraka wa kutokukubaliana na matokeo hayo akidai kuwa yeye alishinda kwa asilimia 62.
Uchaguzi mkuu mwaka 2015 nchini Tanzania ulikuwa wa kihistoria licha ya kuwepo ushindani mkali wa kisiasa lakini pia uliwahusisha wanawake wawili ambao walikuwa wagombea nafasi za juu akiwemo Anne Mngwira, aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya chama cha upinzani cha ACT-Wazalendo na Samia Suluhu Hassan aliyekuwa mgombea mwenza kwa tiketi ya chama tawala cha CCM. Samia anakuwa mwanamke wa kwanza nchini Tanzania kushika nyadhifa ya Makamu Rais.
Taarifa zaidi kuhusu uchaguzi mkuu Tanzania tembelea kwenye tovuti yetu ya www.voaswahili.com