Mawaziri wa mambo ya nchi za nje wa Marekani, Norway na Uingereza wameeleza wasiwasi mkubwa kutokana na kuvunjika kwa mazungumzo baina ya Sudan ya kaskazini na kusini.
Wizara ya mambo ya nchi za nje ya Marekani, ilitowa taarifa ya pamoja ya nchi hizo baada ya mkutano kati ya Bi Hillary Clinton na mawaziri wenzake Jonas Store wa Norway na William Hague wa Uingereza.
Wanadiplomasia hao wamesema ni muhimu kwamba pande zote mbili kuendelea na mjadiliano ambayo serikali ya Sudan kusini iliahirisha Jumapili baada ya kuituhumu Khartoum kufanya njama ya kuipindua serikali ya Kusini na kuuwa watu wake. Serikali ya Kaskazini imekanusha tuhuma hizo.
Mawaziri hao waliwahimiza pia viongozi wa pande hizo mbili kudhibiti makundi yenye silaha chini ya ushawishi wao, katika eneo lenye utajiri wa mafuta la Abyei linalopatikana kwenye mpaka kati ya Kusini na Kaskazini.
Taarifa imeeleza kwamba serikali hizo zimeshaonesha azma ya kufikia amani na ushirikiano wa pamoja na hivyo inabidi ziahidi kwa mara nyingine nia ya kutekeleza makubaliano ya amani ya mwaka 2005.
Mawaziri wa Marekani, Uingereza na Norway walikutana huko Paris ambako mkutano wa mataifa tajiri duniani G8 ulikuwa unafanyika na hasa kufuatia mapigano kati ya majeshi ya serikali ya Sudan Kusini na waasi katika jimbo la Upper Nile mwishoni mwa wiki yaliyosababisha vifo vya watu 42