Wakati Vikosi vya ulinzi na usalama vikiendelea kuimarisha hali ya amani na utulivu visiwani Zanzibar, watu wasiojulikana wanadaiwa kurusha kitu kinachodhaniwa kuwa bomu na kulipua kwenye paa la nyumba ya Kamishna wa Jeshi la Polisi, Zanzibar Bw Hamdan Omar Makame, usiku wa kuamkia Jumanne katika eneo la Kijichi lililoko nje kidogo ya jiji la Zanzibar.
Kamishna Hamdan amesema kuwa shambulizi hilo lilitokea mwendo wa saa tano usiku akiongeza kuwa jeshi lake kamwe halitaruhusu vitendo vya uvunjivu wa Sheria hasa wakati huu kisiwa hicho kinachojiandaa kwa uchaguzi wa marudio. Amesema kuwa uchunguzi umeanza na ana uhakika kuwa waliotekeleza shambulizi hilo watatiwa nguvuni.