Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 15:12

Trump aitoa Marekani katika ushirikiano wa kibiashara


Trump akisaini amri za kiutendaji huko White House
Trump akisaini amri za kiutendaji huko White House

Rais wa Marekani Donald Trump ameanza wiki yake kamili ofisini kwa kuiondoa Marekani kwenye ushirikiano wa kibiashara wa nchi 12 unaojulikana kama Trans-Pacific Partnership (TPP).

Trump pia ameanzisha usitishaji wa ajira kwa idara za serikali kuu na kusisitiza kwa viongozi wa bunge akielezea madai yake kuhusu uchakachuaji wa kura ulimfanya asishinde kura za umaarufu katika uchaguzi wa Novemba.

Katika mkutano uliofanyika White House ukimjumuisha spika wa bunge Paul Ryan, kiongozi wa waliowengi Seneta Mitch McConnel, kiongozi wa wademokrat bungeni Nancy Pelosi na kiongozi wa wademokratik katika Seneti Chuck Schumer, na watu wengine waliokuwa na uzoefu wa mazungumzo hayo, wamesema Trump alidai kuwa kulikuwa na kura zilizochakachuliwa kati ya milioni 3 na milioni 5 zilizopigwa kwa ajili ya Hillary Clinton na wahamiaji haramu.

Hata hivyo kumekuwa hakuna ushahidi wa kutosha kuonyesha kuwa kulikuwa na wizi wa kura katika uchaguzi, na hasa kwa kiwango hicho anachokidai Trump.

Clinton alishinda uchaguzi nchi nzima kwa kura ya umaarufu. Trump ameingia katika utawala kwa sababu ya ushindi mkubwa katika mfumo wa kura za wajumbe (Electoral College) ambayo ndio unaamua nani awe rais.

Trump alikuwa alikuwa akida na kuonya katika muda wa kampeni yake yote kwamba mchakato wa uchaguzi utachakachuliwa dhidi yake. Wiki chache baada ya kuchaguliwa, aliandika katika ujumbe wa Twitter, “ pamoja na kushinda kwa kishindo katika mfumo wa kura za wajumbe, pia nilishinda kwa kura za umaarufu ukitoa wale ambao walipiga kura kinyume cha sheria.”

Trump pia alifanya kampeni dhidi ya makubaliano ya kibiashara ya TPP ambayo yalikuwa yamesimamiwa na rais wa zamani Barack Obama katika awamu yake, lakini haukuidhinishwa na bunge. Ungepitishwa basi ungehusisha biashara kati ya Japan, Australia, New Zealand, Malaysia, Chile, Canada, Mexico na nchi nne nyingine.

Baada ya kusaini amri za kiutendaji Jumatatu zikiitaka Marekani kujiondoa katika TPP na badala yake kuingia katika makubaliano ya kibishara ya nchi kwa nchi, Trump ameliita ni “jambo kubwa kwa wafanyakazi wa Marekani- kile ambacho tumekifanya.”

TPP ingekuwa ni mkusanyiko mkubwa wa kieneo katika makubaliano ya kihistoria ya kibiashara, ambayo yanaunganisha asilimia 40 ya uchumi wa dunia na theluthi tatu ya biashara ya kimataifa.

China haikushiriki katika mazungumzo, lakini inavyoelekea iko tayari kuziba mwanya utakaojitokeza na kuanza kufanya makubaliano na nchi za Kusini mashariki mwa Asia ambazo zilikuwa ziwe sehemu ya makubaliano ya nchi 12.

XS
SM
MD
LG