Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 01:17

Obama apongeza rais mteule Uhuru Kenyatta


Rais mteule Uhuru Kenyatta
Rais mteule Uhuru Kenyatta

Rais mteule Uhuru Kenyatta asema uhusiano wa kidplomasia kati ya Kenya na Marekani utakuwa kati ya viongozi waliochaguliwa kidemokrasia.

Rais mteule wa Kenya Bw. Uhuru Kenyatta na naibu wake Bw. William Ruto, Ijumaa wamekutana na balozi wa Marekani mjini Nairobi Robert Godec ambaye aliwasilisha ujumbe wa pongezi na kheri njema kutoka kwa rais wa Marekani Barack Obama.

Katika ujumbe wake rais Obama alimsihi bwana Kenyatta kuendelea kuongeza nguvu mafanikio yaliyotokana na katiba mpya nchini humo. Bwana Kenyatta alimweleza balozi wa Marekani kuwa mahusiano ya kidiplomasia baina ya Kenya na Marekani yatakuwa kati ya viongozi wawili waliochaguliwa kidemokrasia.

Akiwapongeza Wakenya kwa uchaguzi wa amani, rais Obama alisema Kenya na Marekani ni washirika wakuu tangu Kenya kupata uhuru wake mwaka wa 63.

Naye waziri mkuu anayeondoka Bw. Raila Odinga amesema uamuzi wa mahakama ya juu huko Kenya uliothibitisha kuwa bwana Kenyatta alichaguliwa kwa njia ya haki, ni uamuzi uliokasirisha wengi.

Bwana Odinga aliwaambia umati wa watu katika eneo la Kondele mjini Kisumu kuwa mahakama hiyo ya juu haikutenda haki katika maamuzi hayo. Na kwa matamshi halisi ya bwana Odinga alisema:“mahakama hiyo ishindwe!” Alisema pia kuwa ataendelea kuongoza juhudi za kuleta demokrasia huko Kenya.

Akizungumza na idhaa ya Kiswahili ya Sauti ya Amerika katika Live Talk Ijumaa, mwanasheria na mtaalam wa maswala ya katiba P.L.O. Lumumba alisema hamaki za bwana Odinga ni wazi na kwamba zinatishia kuondoa sifa za juhudi zake kama mtetezi wa demokrasia nchini humo. Bw. Lumumba alisema itakuwa vyema kwa Odinga kuridhika na maamuzi ya mahakama ya juu na kushirikiana na bwana Kenyatta kujenga taifa la Kenya.
XS
SM
MD
LG