Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 21:09

Mvutano mkubwa waendelea kati ya wananchi na Waziri Magufuli.


Mvutano mkubwa waendelea kati ya wananchi na Waziri Magufuli.
Mvutano mkubwa waendelea kati ya wananchi na Waziri Magufuli.

Dk.John Magufuli alitangaza hatua ya kupandishwa kwa gharama hizo na akawaambia wananchi kama watashindwa kukubaliana na ongezeko hilo jipya basi wapige mbizi kwenye bahari ili kuvuka upande wa pili.

Nchini Tanzania wakati huu kunashuhudiwa mvutano mkubwa baina ya serikali na wananchi wanaopinga na kulalamikia hatua ya upandishaji wa ghafla wa nauli kwa ajili ya kivuko cha Kigamboni kilichoko Jijini Dar es salaam.

Katika hali ya kushangaza, waziri wa Ujenzi Dk. John Magufuli alitangaza hatua ya kupandishwa kwa gharama hizo na akawaambia wananchi hao kama watashindwa kukubaliana na ongezeko hilo jipya basi wapige mbizi kwenye bahari ili kuvuka upande wa pili.

Kauli yake hiyo ni kama ametia kaa la moto kwenye mafuta ya petroli kwani pamoja na wananchi hao kugomea nauli hiyo mpya, lakini wanamwinda wakitaka ang'oke madarakani kwa madai kuwa ametoa kauli yenye kebehi.

Tayari wabunge kadhaa kutoka mkoa wa Dar es salaam wamefanya mkutano wa pamoja na kumpa muda wa siku kadhaa waziri huyo kufuta kauli yake hiyo na kuangalia upya kiwango hicho cha nauli.

Watumiaji wa kivuko hicho ambacho ni kiunganisho muhimu kwa wananchi wa rika zote, wanalalamikia nauli hizo mpya wakisema kuwa imezidisha ukali wa maisha.

Wananchi wengi wanahoji kile wanachokiita mafanikio yanayojitokeza kwenye mataifa mengine ambayo huduma za kivuko zinatolewa bure lakini kwa Tanzania bei inaongezeka kila mara.

Wakati huu ambapo bei hiyo mpya inaendelea kutumika, watumiaji wa kivuko hicho wanaendelea kumnyoshea kidole waziri wa Ujenzi Dk. Magufuli.

Kutokana na ongezeko hilo la bei, hivi sasa kunashuhudiwa msururu mkubwa wa magari yakiwa yameegeshwa kando kando ya kivuko na hata wananchi wengine wameanza kupunguza safari za mara kwa mara kutumia kivuko hicho.

XS
SM
MD
LG