Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 14:38

Umoja wa Mataifa Waomba Msaada Kwa ajili ya Wakongo Milioni 6.7


Wakimbizi wa DRC
Wakimbizi wa DRC

Umoja wa Mataifa umeomba msaada wa takriban dola milioni 748 kwa ajili ya kuwapatia msaada wananchi milioni 6.7 huko Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo mwaka huu.

Taasisi hiyo ya dunia pamoja na mamlaka ya Congo wanaomba fedha hizo kwa kile ambacho wanasema ni misaada ya kuokoa maisha ya watu ambao wana shida kubwa katika taifa hilo ambalo limekumbwa na mzozo.

Mzozo wa zaidi ya miongo miwili na kusambaa kwa ukatili kumesababisha mamilioni ya watu nchini DRC kushindwa kukabiliana na hali ya kujikimu kimaisha.

Badala ya hali kuwa nzuri, nchi inazidi kugubikwa na hali mbaya na mahitaji yanaongezeka zaidi. Ombi ambalo limetolewa mwaka huu ni ongezeko la asilimia nane kuliko ombi la awali, na hii inaashiria mkakati mpya wa miaka mitatu.

Msemaji wa ofisi ya mratibu wa Masuala ya Kibinadamu, Jens Laerke, anasema mpango huu mpya unahusisha mwelekeo wa kukabiliana na mizozo inayojitokeza nchini humo.

“Familia, jamii, wanaume, wanawake na watoto nchini Congo ambao wanajaribu kujisaidia, wanakabiliwa na mazingira hatari, na nyingi ya hatari zinasababishwa na kutokuwepo na huduma za msingi au fursa ndogo ya kupata huduma hizo za msingi. Pia kuna mzozo wa ulinzi ambao unahusishwa na mzozo na ghasia, hasa katika maeneo ya mashariki mwa DRC,” amesema msemaji.

Laerke ameelezea kuwa majimbo ya magharibi na kati yanaathirwa kwa ujumla kutokana na umaskini ambao pia unahitaji kutupiwa jicho. Miongoni mwa mambo mengine, amesema fedha ambazo wanaziomba zitawalenga zaidi ya watu milioni mbili waliokoseshwa makazi ndani ya nchi na pia kuwahudumia watoto milioni moja na nusu ambao wamekumbwa na utapiamlo.

Kwa kuongezea nasema maelfu ya watu wanatishiwa na maradhi, magonjwa ya mlipuko na uhaba wa chakula, hasa katika maeneo yenye mizozo.

Anasema sehemu ya fedha hizo zinazoombwa pia zitasaidia katika kushughulikia ongezeko la wakimbizi wanaokimbia mapigano nchini Sudan Kusini. Idara ya Umoja wa Mataifa ya kuhudumia wakimbizi inaripoti kuwa raia 68,000 wa Sudan Kusini wameomba hifadhi nchini DRC. Laerke anasema wakimbizi na jamii wenyeji wanahitaji misaada ya kibinadamu.

XS
SM
MD
LG