Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 13:35

Misri yaanza majadiliano juu ya matumizi ya maji ya Nile


Mto Nile unapita mbele ya jiji la Cairo nchini Misri
Mto Nile unapita mbele ya jiji la Cairo nchini Misri

Tanzania na Misri zimeanza upya majadiliano yanayotaka kuwepo kwa suluhu ya kudumu kuhusu matumizi sahihi ya maji ya Mto Nile.

Tanzania na Misri zimeanza majadiliano hayo, huku kukiwa na shabaha nyingine ya kuzileta pamoja nchi zote zinazopitiwa na mto huo kwa ajili ya kuwa na majadiliano zaidi.

Majadiliano hayo yanakuja katika wakati ambapo nchini Misri kukiwa na utawala mpya, ambao unaanzisha juhudi za kulinda na kuvutia rasilimali zake, baada ya harakati kama hizo kushindwa wakati wa utawala wa rais Hosni Mubarak.

Nchi ambazo zimepitiwa na maji hayo zipatazo saba, miaka michache iliyopita zilianzisha mkataba mpya unaotaka kuwepo kwa uwiano sawa wa matumizi ya maji ya mto, na kuuweka kando mkataba ulioasisiwa na utawala wa kikoloni Uingereza ambao kimsingi ulitoa upendeleo mkubwa kwa nchi za Misri na Sudan.

Mapendekezo mapya yaliyoasisiwa na nchi hizo saba, yaliyosainiwa katika mkutano wa mawaziri wa Maji uliofanyika Kampala, nchini Uganda, yalipingwa vikali na nchi hizo mbili, Misri na Sudan na hivyo kuzusha hali ya wasiwasi juu ya majaliwa na mto huo.

Hata hivyo kutokana na utete wa suala hilo, Waziri wa mambo ya Nje wa Misri Mohamed Kamel Amr hivi sasa ameanza safari ya kuzitembelea nchi zinazopitiwa na maji yam to huo kwa ajili kuweka ushawishi kabla nchi hizo hazijakutana wiki ijayo huko Nairobi Kenya.

Kwa kuzingatia kauli ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania Bwana Bernard Membe, kuna uwezekano sasa pande hizo zikafikia makubaliano yatayozingatia maslahi ya pande zote.

Kuhusu hali ya siasa nchini Misiri ambayo hivi karibuni kulizuka hali sokomoko kufuatia hatua utawala wa kijeshi kuendelea kusalia madarakani baada ya kuondolewa kwa rasi Hosni Mubarak, waziri Membe aligusia eneo hilo akisema kuwa kwa hivi sasa kuna maendeleo mazuri na ya kuridhisha.

XS
SM
MD
LG