Mke wa Rais wa Marekani, Michelle Obama yupo Johannesburg Afrika kusini, ambako amekutana na shujaa wa kupambana na ubaguzi wa rangi nchini humo Nelson Mandela.
Bibi Obama amekutana na Rais huyo wa zamani mwenye umri wa miaka 92, nyumbani kwake, baada ya kutembelea ofisi za taasisi ya Mandela.
Ikiwa kwenye matembezi hayo, familia ya Obama imeangalia vitu kadhaa kama vile dawati la Mandela akiwa gerezani na vijitabu vyenye maandishi yake.
Bibi Obama yupo katika ziara ya wiki moja barani Afrika, ambapo atahamasisha vijana kujituma. ameambatana na watoto wake wa kike, Malia na Sasha, pamoja na mama yake mzazi, Marian Robinson.
Bi Obama aliwasili katika mji mkuu Pretoria jumatatu na jumanne asubuhi alikutana na mmoja wa wake wa Rais Jacob Zuma, Nompumelelo Zuma.