Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 20:02

Mapigano yaendelea Jamhuri ya Afrika ya Kati


Wapiganaji wa kundi la Seleka wakifanya doria mjini Bangui
Wapiganaji wa kundi la Seleka wakifanya doria mjini Bangui
Serikali ya Jamhuri ya Afrika ya Kati inasema watu 60 wameuwawa katika mapigano kati ya wapiganaji wanaomuunga mkono rais aliyetimuliwa madarakani Francois Bozize na waasi wanaoshikilia madaraka.

Msemaji wa serikali Guy Simplice Kodegue anasema mapigano hayo yalitokea Jumamosi na Jumapili katika mji wa kaskazini magharibi wa Bossangoa nyumbani kwa Bw. Bozize.

Umoja wa Mataifa unasema asilimia 80 ya watu wa mji huo ambao wanakisiwa kuwa 30,000 wamekimbilia porini na maeneo mengine.
Maafisa wa Umoja wa Mataifa wanasema wafanyakazi wake wawili ni miongoni mwa waliouawa katika ghasia hizo.

Mapigano hayo yalikuwa kati ya makundi ya wanamgambo na kundi mseto la waasi wa Seleka ambao walihitimisha utawala wa miaka 10 wa rais Bozize mwezi Machi . Kundi hilo la Seleka linajaribu kufanya mabadiliko ya kisiasa ili kuandaa uchaguzi mkuu wa kitaifa katika muda wa miezi 18 ijayo.

Kufikia sasa Umoja wa Mataifa unasema ghasia katika taifa hilo zimesababisha wananchi wapatao 62,000 kutafuta hifadhi nje ya nchi tangu mwanzo wa mwezi huu wa Septemba.

Jamhuri ya Afrika ya Kati imekumbwa na msururu wa mapinduzi ya serikali na maasi tangu ilipopata uhuru wake kutoka Ufaransa mwaka wa 1960.
XS
SM
MD
LG