Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 04:02

Mafuriko yaathiri wengi Msumbiji


Picha inayoonyesha barabara iliyosombwa na mafuriko katika eneo la Chokwe, Msumbiji, Januari 30, 2013.
Picha inayoonyesha barabara iliyosombwa na mafuriko katika eneo la Chokwe, Msumbiji, Januari 30, 2013.

Takriban watu robo milioni wameathiriwa na mafuriko. Shirika la Msalaba Mwekundu lahofia kuzuka magonjwa ya Malaria na kipindupindu.

Shirika la kimataifa la Msalaba Mwekundu na Ilali Nyekundu linasema linahitaji takriban dola laki 7 kama msaada wa dharura kwa waathiriwa wa mafuriko huko Msumbiji. Takriban watu robo millioni wameathiriwa na mafuriko yanayoendelea, huku ikikadiriwa kuwa takriban watu laki moja na elfu 40 wamepoteza makazi yao.

Haya ni mafuriko mabaya zaidi kuwahi kuathiri Msumbiji kusini na kati tangu mwaka 2000, pale zaidi ya watu 700 walipofariki na wengine milioni moja kupoteza makazi yao.

Chini ya watu mia moja wamefariki katika mafuriko ya mwaka huu. Shirika la Msalaba Mwekundu linasema idadi hiyo ndogo ya vifo inaashiria kuwa mradi wa kutoa onyo mapema na kuzuia maafa unafanya kazi vyema.

Hata hivyo mvua kubwa zimesababisha uharibifu mkubwa kwa nyumba, mashule, mimea na hata vituo vya afya, na hivyo kuwalazimu raia walioathiriwa kuacha makazi yao na kwenda kutafuta hifadhi kwingine. Mvua zinabashiriwa kuendelea hadi mwezi Aprili.

Msemaji wa shirika la Msalaba Mwekundu Jessica Sallabank, anasema eneo la Gaza ni mojawapo ya jimbo liloathiriwa zaidi na kwamba watu laki moja katika jimbo hilo wamepoteza makazi yao na wengi wanalala nje au vichakani.

Takriban watu elfu 40 wanaishi kwenye kambi za muda katika mji wa Chokwe. Anasema pia kuwa kuna uwezekano wa kuzuka maradhi ya Malaria na kipindupindu .


XS
SM
MD
LG