Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 21:29

Oscar Ilojichanganya Kuliko Zilizo Tangulia?


Jimmy Kimmel and Warren Beatty wanacheka baada ya kusahihisha kosa katika kuitangaza tuzo ya filamu bora ya Oscar
Jimmy Kimmel and Warren Beatty wanacheka baada ya kusahihisha kosa katika kuitangaza tuzo ya filamu bora ya Oscar

Tuzo ya Oscar imeandika historia Jumapili baada ya kwenda “mrama” kwa dakika kadhaa.

Kikundi kilichotengeneza filamu ya “Moonlight” kiliibuka na ushindi uliowashtua wengi lakini kabla ya kutangazwa, kundi lililotengeneza filamu ya “La La Land” lilichukuwa tuzo hiyo ambayo ilidumu kwa dakika chache kabla ya watazamaji kupatwa na butwaa katika kinyang'anyiro cha tuzo ya filamu bora.

Watangazaji wa tuzo ya Oscar, Warren Beatty na Faye Dunaway, usiku wa Jumapili, huko Los Angeles, bila ya kukusudia walimtangaza mshindi kwa makosa na ghafla ushindi ule kurejeshwa kwa “Moonlight.”

Wakati ushindi huo ukitangazwa kwa makosa kwamba ni wa “La La Land” katika sinema bora, waigizaji na watayarishaji wa picha ya “La La Land” walikuwa tayari wameshafika jukwaani na kuanza kutoa hotuba ya kukubali zawadi hiyo mara tu wakitahamaki kuwa “Moonlight” ndio imechukuwa ushindi.

PricewaterhouseCoopers, kampuni ya fedha iliyopewa jukumu la kusimamia bahasha zenye majina ya washindi waliomba radhi kwa kosa lao na kusema tayari “wamesha rekebisha kosa hilo mara moja.”

Hatimaye Barry Jenkins mwenye filamu ya “Moonlight” ilishinda tuzo ya Academy Awards katika tukio la kihistoria, japokuwa mkanganyiko huo wa kosa la kumtaja mshindi asiyestahili lililowasikitisha wengi na kuleta mkang’anyiko uliokuwa haujatarajiwa.

Tuzo ya Oscar ni tuzo za Sanaa ya filamu na sayansi zitolewazo kila mwaka na taasisi ijulikanayo kama AMPS. Ilianza kwa mara ya kwanza 1929 katika hoteli maarufu ya Hollywood Roosevolt. Kwa mara ya kwanza ilitangazwa kwenye televisheni mwaka 1953. Hivi leo inaonekana moja kwa moja katika nchi 225 duniani.

Wakati lilipotokea kosa Jumapili kwenye tamasha hilo, jina la Steve Harvey lilisambaa katika mitandao, kukumbusha kwamba tatizo kama hili liliwahi kutokea wakati wa shindano la Miss Universe 2015. Lakini mara moja aliomba radhi kwa kosa hilo. Na hivyo Miss Colombia Ariadna Gutierrez kuachia taji hilo kwa kulisalimisha kwa Miss Philippines Pia Wurtzbach ambaye alikuwa ameibuka mshindi.

Jumapili, watangazaji Warren Beatty na Faye Dunaway walichukua bahasha iliyokosewa- ambayo ilikuwa ya mshindi mwigizaji mwanamama bora Emma Stone- ambaye alikuwa ameshinda nafasi ya mwigizaji bora. Baada ya kugundua imekosewa, wasimamizi wanaozichambua kura; PriceWaterhouseCoopers walikimbilia jukwaani kusitisha hotuba ya kukubali tuzo kwa kundi lilokuwa halijashinda.

Lakini nyuma ya jukwaa, Stone amesema kuwa alikuwa ameshikilia bahasha wakati huo. “Nafikiri kila mtu bado yuko katika hali yakuchanganyikiwa,” amesema Stone. Baadae muigizaji huyo ambaye alithibitisha anaipenda kwa dhati “Moonlight,” aliongeza kusema, “Je hii Oscar ni iliyo changanyikiwa kuliko wakati wowote mwengine."

Hata hivyo kulikuwa na mshtuko uliowaudhi wengi kwamba “La La Land” walipata kupendekezwa mara 14, rekodi ambayo inawalinganisha na “Titanic” and “All About Eve.”

Barry Jenkins kijana anayeinukia katika zama za uigizaji alipata tuzo ndogo ya Oscar ya dola milioni 1.5.
“Hata katika ndoto zangu sitaki kuamini ni kweli imetokea,” alisema Jenkins aliyekuwa ameshangazwa na ushindi wake.

Jimmy Kimmel, Muongozaji wa tamasha alikuja mbele mara moja kukifahamisha kikundi kwamba “Moonlight” ndio waliokuwa wameshinda, na kuwaonyesha kile kilichokuwa ndani ya bahasha kama ushahidi.

“Nilijua kwamba nimeharibu,” alisema Kimmel, muongozaji kwa mara ya kwanza. “Naahidi sitorudi tena.”

Lakini kwa ustaarabu kabisa mtayarishaji Jordan Horwitz hapo kwa upole alitoa tuzo kumpa mtayarishaji wa “Moonlight.”

Mpaka kumalizika kwa tatizo hilo, matangazo yaliendelea kubadilika badilika, yakionyesha kati ya malalamiko dhidi ya Donald Trump na mabishano yenye hisia kali juu ya watu wote kutendewa haki, huku tuzo hizo zikienda kati ya vikundi vya “La La Land,” “Moonlight” na “Manchester by the Sea.”

Ushindi wa Viola Davis, ambaye alikuwa ni mmoja wa waigizaji wakuu wawili katika filamu ya "Fences" iliyochezwa na Denzel Washington iliyochukuliwa kutoka katika igizo lake August Wilson ulitarajiwa. Pia Mahershala Ali, mchezaji mwenza mkuu wa “Moonlight,” alitarajiwa kushinda na watu wengi.

Lakini malalamiko ya wazi yalitolewa na mmoja wa washindi aliyekuwa hajahudhuria tamasha hilo.

Filamu ya nje bora kwa mara ya pili imekwenda kwa Asghar Farhadi, mkurugenzi wa Iran alotengeneza filamu ya “ A Salesman.”

Amesema hakuhudhuria tamasha hilo kwa sababu ya katazo la kusafiri la Trump lililotolewa kwa nchi saba zenye Waislamu wengi. Anousheh Ansari, Mwanaanga wa Kiiran alisoma risala yake Farhadi.

“Nasikitika sijaweza kuwa pamoja na nyinyi usiku huu,” imesema risala yake.

“Kutokuwepo kwangu ni kutokana na kuwaheshimu wananchi wa taifa langu na wale wa mataifa sita mengine ambao wamevunjiwa heshima na sheria isiyo ya kibinadamu ambayo inakataza wahamiaji kuingia Marekani.”


XS
SM
MD
LG