Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 18:16

Kesi ya Ghailani huwenda ikamalizika mapema


Naibu mwendesha mashtaka wa Marekani Nicholas Lewin, fakitoa hoja yake kwenye kesi ya Ahmed Khalfan Ghailani, kushoto, huko New York.
Naibu mwendesha mashtaka wa Marekani Nicholas Lewin, fakitoa hoja yake kwenye kesi ya Ahmed Khalfan Ghailani, kushoto, huko New York.

Kesi ya Mtanzania Ahmed Ghailani huko New York, anaetuhumiwa kwa kupanga njama ya mashambulio ya mabomu dhidi ya ubalozi wa Marekani huko Nairobi na Dra es Salaam, 1998 huwenda ikamalizika mapema kuliko ilivyotazamiwa. Waendesha mashtaka wanasema watakamilisha kesi yao katika muda wa wiki chache zijazo. Na huwenda kesi ikamalizika mwishoni mwa disemba.

Waendesha mashtaka walianza kesi wiki hii kwa kuwaita mashahidi wawili kutoka Mombasa Kenya, ambao wanalifahamu sana duka la nguo la Azzam. Ghailani alifanya kazi katika duka hilo mwaka 1997 na 1998, na wapelelezi wa FBI waligundua ushahidi wa chembe chembe ya miripuko ndani ya duka hilo.

Shahidi moja alikua fundi wa magari na gereji yake ilikua upande wa pili wa barabara kutoka duka hilo. Alitoa ushahidi kwamba wanaume kadha walikwenda kwenye duka hilo miezi saba kabla ya shambulio.

Akijibu suala la mwendesha mashtaka ikiwa wanaume hao walisimama nje ya duka, alisema, kiswahili chao hakikua kizuri sana na walizungumza kwa lafdhi ya ki-Tanzania.

Shahidi mwengine alikua Salim Ahmed Swedan, kakake mkubwa Sheikh Ahmed Salim Swedan, mtu anaetuhumiwa kwa kutoa lori zilizotumiwa kusafirisha mabomu hadi ubalozi wa Marekani huko Nairobi na Dar es Salam. Salim alitoa ushahidi kwamba kakake mdogo alikua rafiki wa mtu aliyesimamia duka hilo la nguo ambalo lilikua la mamake.

Shahidi alisema wiki moja kabla ya shambulio la Nairobi kakake alimuambia anawahamisha mkewe na watoto wake watatu kutoka Mombasa hadi Yemen. Swedan mdogo inaripotiwa, aliuliwa na shambulio la kombora kutoka ndege ya Marekani isiyokua na rubani huko Pakistna mwaka jana.

Wachunguzi wawili wa FBI walopelekwa kuchunguza mripuko wa Nairobi walitoa pia ushahidi wao hiyo jana. Mpelelezi maalum Megan Miller alisema, FBI iligundua ushahidi wa chembechembe za miripuko kwenye duka la nguo.

Mtaalamu wa miripuko Donald Sachtleben alisema, anakadiria huwenda kulikuwepo kwa uchache kiasi ya kilo 460 za miripuko ya aina ya TNT iliyotumiwa katika shambulio la Nairobi.

Mwendesha mashtaka alimuliza Sachtleben ikiwa anatambua vipande vizito vya vyuma vilivyo kunjika vilivyopatikana kwenye vifusi vya mripuko. Alisema ni nguvu za kupita kiasi pekee ndizo zingeliweza kukunja na vyuma vinene kama hivyo.

Wakati wa zamu ya upande wa watetezi kuwahoji mashahidi wa upande wa mashtaka, mawakili waliuliza masuala ya kiufundi pekee yake.

XS
SM
MD
LG