Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 12:35

Kesi ya ugaidi dhidi ya Ghailani yaanza New York.


Mtuhumiwa mashambulio ya kigaidi Ahmed Khalfan Ghailani, kushoto, akiwa mahakamani
Mtuhumiwa mashambulio ya kigaidi Ahmed Khalfan Ghailani, kushoto, akiwa mahakamani

Kesi dhidi ya mtuhumiwa wa ugaidi Ahmed Ghailani inaanza mjini New York Jumanne. Ghailani anashtakiwa kwa kuhusika na mashambulizi ya mabomu katika Ubalozi wa Marekani nchini Tanzania na Kenya mwaka wa 1998.

Kesi hiyo ilianza kwa taarifa kutoka kwa naibu mkuu wa sheria wa Marekani Nicholas Lewin, aliyeleza kuwa serikali itaonyesha mshtakiwa alihusika katika ununuzi wa gari lililohifadhia vifaa vya ulipuaji vilivyotumika katika mashambulizi ya mabomu ya wahanga wa kujitolea mjini Dar-es-salaam, Tanzania.

Lewin alisema namba za usajili za gari hilo ziliwapelekea wapelelezi kubaini kuwa Ghailani alihusika na kwamba waligundua chembechembe za vilipuaji katika chumba chake.

Serikali ya Marekani katika kesi hii inataka kuonyesha kuwa ina ushahidi kwamba Ghailani alikimbilia Pakistan na washirika wenzake kutoka kundi la kigaidi la al-Qaida akitumia jina bandia na pasi bandia ya kusafiria siku moja kabla ya shambulizi hilo.

Mmoja wa mawakili wa Ghailani Steve Zissou anasema mshtakiwa alikuwa kijana mdogo wakati wa mashambulizi hayo, na kwamba aliishi na wanachama wa al-qaida waliomzidi umri na kuwaheshimu sana akiwaona kama wafanyibiashara walioimarika.

Jaji Kaplan anaoyeongoza kesi hiyo anasema huenda kesi hii ikachukua wiki kadhaa au hata miezi, na kuingia katika mwaka ujao.

Kesi ya Ghailani ni ya mshtakiwa wa kwanza aliyezuiliwa katika jela la Guantanamo Bay nchini Cuba, kusikilizwa katika mahakama ya kiraia ya Marekani.

XS
SM
MD
LG