Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 05:22

Kenya yapeleka wajumbe Somalia kwa ajili ya kuachiliwa mtalii wa kifaransa


Watali wakitembea katika barabara kuu ya Lamu, Kenya
Watali wakitembea katika barabara kuu ya Lamu, Kenya

Kenya imepeleka wajumbe Somalia ili kujadili kuachiliwa huru mtalii wa kifaransa aliyetekwa nyara Jumamosi kutoka katika nyumba yake ya mapumziko karibu na Lamu.

Afisa wa usalama wa serikali ya Kenya asiyetaka kutambuliwa jina lake amesema Jumapili kwamba, serikali imepeleka wajumbe Somalia kuanza mawasiliano na watekaji nyara.

Mtali huyo mlemavu kutoka Ufaransa aliyetajwa kuwa ni Marie Dedieu, alitekwa nyara Jumamosi asubuhi kutoka nyumba ya mapumziko katika kisiwa cha Manda karibu na mji wa Lamu.

Watekaji nyara hao walipambana na vikosi vya usalama vya Kenya kabla ya kukimbia na Dedieu hadi Somalia. Hii ni mara ya pili kwa mtalii kutekwa nyara katika eneo hilo katika kipindi cha wiki tatu na washambulizi wa Kisomali.

Mwezi uliopita mtalii mmoja wa Uingereza Judith Tebutt alitekwa nyara kaskazini ya Lamu baada ya mumewe kuuliwa na washambulizi wa Kisomali. Hadi hii leo inaripotiwa anashikiliwa kati kati ya Somalia.

Waziri wa Utali wa Kenya, Najib Balala, anasema atatembelea eneo hilo Jumatatu pamoja na mkuu wa usalama nchini humo kutathmini hali ya mambo na kuwahakikishia wakazi na wafanyabiashara kwamba kuna usalama katika eneo hilo.

XS
SM
MD
LG