Mwandishi wa habari aliyekamatwa na polisi Jumanne usiku mjini Nairobi sasa ameachiliwa huru baada ya kuhojiwa na maafisa wa idara ya Upelelezi kuhusu madai ya kuchapisha habari za matumizi mabaya ya fedha za serikali katika Wizara ya Usalama wa ndani. Lakini waandishi wengine wawili nchini Kenya wanasakwa na polisi kuhusiana na madai hayo.
Mwandishi huyo wa habari John Ngarachu alikamatwa na polisi nje ya majengo wa bunge kuhusu na habari alizochapisha Ijumaa iliyopita kuhusu matumizi mabaya ya fedha za umma katika wizara inayohusika na Usalama wa ndani, inayosimamiwa na Waziri John Nkaissery.
Baada ya habari hizo kuenea Jumanne usiku,viongozi,waandishi wa habari na wananchi kwa jumla waliilani serikali kwa kumtia nguvuni mwaandishi huyo na kusema ni mwanzo wa serikali ya Rais Kenyatta kuangamiza uhuru wa uandishi wa habari.
Kulingana na Waziri Nkaissery,mwaandishi huyo John Ngarachu alitiwa nguvuni kwa kuandika habari za siri ya serikali kuhusu matumizi ya fedha za wizara hiyo.Alitakiwa kutoa taarifa ya kuthibitisha chanzo au chemichemi ya habari hizo-kinyume na maadili ya uandishi wa habari.