Kenya imewatuma maafisa zaidi wa usalama katika kaunti ya Lamu ambako watu waliokuwa na bunduki waliwaua watu watatu Jumapili na kuwajeruhi wengine kadhaa na kuzua khofu zaidi ya mashambulio ya kigaidi.
Ripoti ya Idara ya polisi nchini humo ilithibitisha waliouawa ni watu watatu, lakini ikasema ni mapema mno kuhusisha mauaji hayo na kundi la kigaidi la Al Shabaab kutoka Somalia.
Wakati huo huo watu wameripotiwa kutoroka kutoka kijiji cha kaisari mahala ambapo mauaji hayo yalitokea pamoja na vijiji vya jirani ambako watu wengine wameonekana wakihamisha mifugo yao kwa kuhofia usalama wa mali na familia zao.