Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 13:38

Kamanda wa M23 akamatwa Uganda


Wanajeshi wa DRC washerekea ushindi dhidi ya M23 huko DRC
Wanajeshi wa DRC washerekea ushindi dhidi ya M23 huko DRC
Maafisa wa jeshi la Uganda wamethibitisha kwamba kamanda wa kundi la waasi la M23 la Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo, Sultan Makenga amejisalimisha na anashikiliwa na Uganda. Hata hivyo maafisa hao hawajaeleza bayana mahala kamanda huyo anashikiliwa kwa wakati huu.

Hatua hiyo ya kundi la M23 kutangaza kwamba linaweka chini silaha zake na hapo siku ya Alhamisi kutangazwa kujisalimisha kwa kamanda wake Sultan Makenga kwa maafisa wa Uganda kunachukuliwa kuwa ushindi mkubwa kwa jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo- FARDC.

please wait

No media source currently available

0:00 0:05:26 0:00
Kiungo cha moja kwa moja

Ushindi wa FARDC unatokana na msaada mkubwa kutoka majeshi ya kulinda amani ya Umoja wa Mataifa huko Congo-MONUSCO na kikosi kipya cha kuingilia kati cha kikanda kinachoongozwa na Tanzania.

Hata hivyo wachambuzi wanaonya dhidi ya kuwa na matumaini makubwa katika kupatikana amani ya kudumu kwa wakati huu huko mashariki mwa taifa hilo la Afrika ya Kati lenye utajiri mkubwa wa madini.

Akifuatana na ujumbe wa Umoja wa Mataifa na wajumbe wa mataifa mengine Gavana wa jimbo la Kivu Kaskazini, Julien Paluku walitembelea moja wapo ya ngome kuu ya M23 ya huko Chanzu kwenye mpaka na Uganda. Anasema hivi sasa mazungumzo ya Kampala yatachukua sura nyingine kabisa.

“Kitu ambacho kitatuletea amani, baada ya kuwapiga hawa watu wa M23, inabidi hivi sasa kuwapiga wapiganaji wa FDLR na vikundi vya ADF-Nalu vya Uganda na makundi yote ya Mai Mai, ili kuhakikisha kwamba nchi yetu ya Kongo imerudia na usalama. Tukiendelea kuzungumza nawatu haitatupatia muda ya kuyapiga yale makundi mengine. Na sidhani kuzungumza na Bisima na Makenga itaweza kutuletea amani”.

Jumuiya ya Kimataifa imepongeza matokeo hayo. Mjumbe maalum wa Marekani kwa ajili ya Kanda ya Maziwa Makuu, Russ Fiengold anasema habari za kujisalimisha kwa M23 ni jambo zuri. “Hii ni hatua muhimu kabisa katika utaratibu wa kuhakikisha kwamba kitisho hichi chote dhidi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kimekamilika na hivi sasa kusonga mbele katika masuala mengine ya kujaribu kuhakikisha kwamba kuna amani na ustawi katika Kanda ya Maziwa Makuu.”

Feingold anasema hivi sasa cha muhimu ni kupanga mipango ya kuwapokonya silaha wapiganaji wa M23 kufuatia uwamuzi wao wa kumaliza vita. Anasema baadhi yao wanaweza kupewa msamaha.

Jeshi la Congo lilipambana na wapiganaji wa M23 kwa karibu miezi 18 likiwa moja wapo ya makundi matano makuu yanayoendesha shughuli zao huko mashariki ya taifa hilo.

Bwana Feingold anasema mazungumzo yanayohitajika kufanyika hivi sasa yanabidi kuhusisha mataifa yote ya kanda na hasa kushughulikia matatizo ya msingi yanayovuruga utulivu huko jamhuri ya kidemokrasi ya Congo- DRC.
XS
SM
MD
LG