Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 11:52

Hosni Mubarak yupo mahututi


Rais wa zamani wa Misri, Hosni Mubarak
Rais wa zamani wa Misri, Hosni Mubarak

Hosni Mubarak aliitawala Misri kwa takribani miaka 30 hadi alipoondolewa madarakani kufuatia ghasia zilizozuka nchini humo Februari mwaka 2011

Vyanzo vya usalama nchini Misri vinasema Rais aliyeondolewa madarakani Hosni Mubarak yupo mahututi kwenye mashine ya kupumulia baada ya kukimbizwa kutoka jela kwenda hospitali ya kijeshi kutokana na kiharusi.

Ripoti za awali kutoka shirika la habari la taifa-MENA zilisema madaktari wa Mubarak walitangaza kuwa kiongozi huyo wa zamani “kitabibu alikuwa amekufa” wakati alipowasili kwenye hospitali ya Maadi kusini mwa Cairo baada ya kuhamishwa kutoka jela ya Torah.

Ripoti inasema madaktari walishindwa kumrejesha katika hali ya kawaida Mubarak baada ya kushindwa kupumua. Maafisa wa kijeshi walikiri mapema Jumatano kwamba Mubarak anasumbuliwa na kiharusi lakini walisema kwa sasa anatumia mashine ya kupumulia na kwamba ni mapema mno kusema kitabibu amekufa.

Wakati huo huo Mubarak mwenye umri wa miaka 84 alitawala Misri kwa takribani miaka 30 hadi alipoondolewa madarakani kufuatia wimbi la maandamano makubwa ya siku 18 yaliyofanyika Februari mwaka 2011.

Mtoto huyo wa kiume wa afisa mmoja wa wizara ya sheria alipanda cheo katika jeshi la anga la Misri na hatimaye kuwa kamanda na naibu waziri wa ulinzi. Mubarak alitangazwa kuwa naibu wa Rais Anwar Sadat mwaka 1975 na alikuwa pembeni yake wakati Sadat alipouwawa mwezi Oktoba mwaka 1981 na wanamgambo wa ki-Islam.




XS
SM
MD
LG