Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Aprili 23, 2024 Local time: 19:21

Dunia yaadhimisha siku ya ukimwi


Maelezo mbali mbali katika maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani
Maelezo mbali mbali katika maadhimisho ya Siku ya Ukimwi Duniani

Disemba mosi ni siku ya ukimwi duniani. Katika miaka 35 ya janga la ukimwi kiasi cha watu milioni 80 wameambukizwa na HIV na takribani milioni 40 wamefariki kutokana na ugonjwa huo. Lakini mafanikio mazuri yameonekana katika miaka ya karibuni katika kuzuia na kutibu ugonjwa huo. UNAIDS, program ya Umoja wa Mataifa inayoshughulikia HIV na Ukimwi imeweka lengo la kutokomeza uambukizaji wa ugonjwa huo ifikapo mwaka 2030.

Katika ujumbe kwa njia ya video kuadhimisha siku ya ukimwi Duniani, ambayo ni Disemba mosi, Mkurugenzi Mkuu wa UNAIDS, Michel Sidibe aliwaomba watu kuwakumbuka wale waliopoteza maisha kutokana na ugonjwa wa Ebola. “Ebola inatukumbusha sisi kile tulichokabiliana nacho mwanzoni mwa vita dhidi ya HIV. Watu walikuwa wakijificha. Walikuwa na wasiwasi. Unyanyapaa, ubaguzi. Tulikuwa hatuna matumaini yeyote”

Michel Sidibe
Michel Sidibe

Sidibe alisema kwamba shukran kwa ushirikiano wa kimataifa kuhamasisha jamii na uwanaharakati wa makundi yasiyo ya kiserikali , tumeweza kuligeuza janga hili na kuleta mafanikio. Anasema maisha ya mamilioni ya watu walioambukizwa na HIV yameokolewa kutokana na kupatikana kwa dawa za ARVs.

UNAIDS hivi sasa ina kile inachokiita mkakati wa FAST TRACK wa kumaliza mlipuko huu ifikapo mwaka 2030. Awamu ya kwanza inaweka malengo kwa mwaka 2020 ambayo inajulikana kama 90-90-90.

Mitchell Warren ni Mkurugenzi Mtendaji wa HIV kwenye kundi la wanaharakati liitwalo AVAC. “Tulipokuwa kwenye mkutano wa ukimwi wa mwaka huu huko Melbourne, Australia, UNAIDS ilizungumzia kuhusu lengo hili la kupata asilimia 90 ya watu ambao wameathirika na HIV, kujua hali yao kiafya, asilimia 90 ya hao wanapatiwa matibabu na asilimia 90 ya wale wanaopata matibabu, wafikie kile tunachoeleza kupunguza virusi. Yani dawa za ARVs zitapunguza kabisa virusi mwilini.”

Mgonjwa wa HIV akionesha dawa za ARV
Mgonjwa wa HIV akionesha dawa za ARV

Utafiti unaonesha kwamba pale virusi zaidi vya HIV vinapungua katika mwili na hivyo basi inapunguza sana uwezekano wa aliyeathirika kumuambukiza mtu mwingine.

Warren alisema matibabu pekee hayatoshi kufanikisha ukweli wa mpango wa 90-90-90. Kiongozi wa AVAC anasema kinga inabidi kupewa kipaumbele Zaidi katika mkakati wa UNAIDS.

“Tunahitajika kuhakikisha kwamba tuna malengo thabiti ya wazi na rasilmali pamoja na miradi ambayo inaweka juu kiabisa kinga katika kipaumbele chake pamoja na matibabu, hivyo basi tunaweza kufikiria kuhusu kutokomeza ugonjwa huo.”

Alisema mipango mikubwa kama 90-90-90 inaweza kugharimu fedha nyingi jambo ambalo anasema ni vigumu kupata siku hizi.

XS
SM
MD
LG