Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 10:30

Burundi yawazuia wachunguzi wa UN kuingia nchini humo


Ghasia za kisiasa Burundi zilizopelekea wachunguzi wa UN kuzuiwa kuingia huko
Ghasia za kisiasa Burundi zilizopelekea wachunguzi wa UN kuzuiwa kuingia huko

Serikali ya Burundi imewapiga marufuku wachunguzi wa kitengo kinachoshughulika na masuala ya haki za binadamu katika Umoja wa Mataifa kuingia nchini humo kufuatia kutolewa kwa ripoti ambayo inaeleza ukiukwaji mbaya wa haki za binadamu katika nchi hiyo iliyopo Afrika mashariki.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Associated Press-AP barua iliyotolewa Jumatatu iliyotiwa saini na waziri wa mambo ya nje wa Burundi, Alain Aime Nyamitwe, ilisema wachunguzi wa Umoja wa Mataifa, Pablo de Greiff raia wa Colombia, Christof Heyns wa Afrika kusini na Maya Sahli-Fadel wa Algeria hawaruhusiwi kuingia nchini humo.

Wachunguzi hao kutoka kitengo kinachohusika na masuala ya haki za binadamu katika Umoja wa Mataifa wanahusishwa na ripoti iliyotolewa mwezi uliopita ambayo inawashutumu maafisa wa serikali ya Burundi kwa ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu unaowalenga wapinzani wa serikali.

Msemaji wa Umoja wa Mataifa, Stephane Dujarric, alizungumza huko New York nchini Marekani na alitoa wito kwa Burundi kuendelea kushirikiana na wachunguzi hao wa haki za binadamu.

XS
SM
MD
LG