Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 13:30

Burundi yaendelea na uchaguzi leo


Wapiga kura wakiwa kwenye mistari tayari kuingia ndani ya kituo cha kupiga kura
Wapiga kura wakiwa kwenye mistari tayari kuingia ndani ya kituo cha kupiga kura

Serikali ya Burundi imeendelea na uchaguzi wa bunge jumatatu licha ya upinzani kususia na ukosoaji kutoka Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika wakihoji ikiwa kuna mazingira ya upigaji kura kwa njia ya huru na haki.

Mkuu wa Umoja wa Afrika, Nkosazana Dlamini Zuma alielezea wasi wasi kuhusu kile alichokiita “hali mbaya sana ya kisiasa na usalama” nchini Burundi na alisema waangalizi wa Umoja wa Afrika hawatahudhuria katika uchaguzi wa jumatatu.

Alisema viongozi wa AU, UN na kieneo waliiomba Burundi kuchelewesha upigaji kura hadi Julai 30 pamoja na upigaji kura wa rais ambao hivi sasa umepangwa kufanyika Julai 15, lakini serikali haijakubali kufanya hivyo. Alisema Burundi ipo katika hatua mbaya ya historia yake na kwamba vuguvugu la kisiasa limeibua hali mbaya ya amani na usalama katika nchi na eneo zima.

Rais Pierre Nkurunziza
Rais Pierre Nkurunziza

Uamuzi wa Rais Pierre Nkurunziza wa kuwania awamu ya tatu madarakani ulichochea jaribio la mapinduzi lililoshindikana mwezi uliopita na kuendeleza kukosolewa kutoka kwa watu ambao walisema anakiuka ukomo wa mihula miwili uliopo katika katiba. Mahakama ya katiba nchini Burundi ilielezea kwamba bwana Nkurunziza anastahili kwa sababu awamu ya kwanza ya muhula wake madarakani alichaguliwa na bunge na si wapigakura hapo mwaka 2005.

Mvutano umezusha ghasia hususani katika mji mkuu Bujumbura mahala ambapo mashahidi walisema jumapili kwamba watu wawili walikufa kutokana na mapambano ya usiku kucha. Ghasia pia zimelazimisha zaidi ya raia wa Burundi 100,000 kukimbilia nchi za jirani.

Ban Ki-Moon
Ban Ki-Moon

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon alitoa wito kwa viongozi wa Burundi hapo Jumapili kufikiria maslahi makubwa ya watu wa nchi hiyo na kutatua masuala ya kisiasa kupitia mashauriano ili kuweza kuleta amani na kuboresha maridhiano ya kitaifa.

XS
SM
MD
LG