Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Aprili 23, 2024 Local time: 19:07

Besigye na viongozi wengine wafikishwa mahakamani Uganda


Kiongozi wa upinzani nchini Uganda, Kizza Besigye
Kiongozi wa upinzani nchini Uganda, Kizza Besigye

Dr.Besigye na wenzake wanne walifikishwa mahakamani lakini raia tisa wengine waliohusishwa na shutuma za mauaji hawakutokea

Rais wa chama cha upinzani cha FDC nchini Uganda, Dr.Kizza Besigye na viongozi wengine watatu wa kisiasa akiwemo mbunge wa wanawake mjini Kampala Nabillah Sempala, meya wa Kawempe, Mubarak Munyagwa na Ingrid Turinawe kiongozi wa wanawake wa chama cha FDC, Jumatano walifikishwa mahakamani kujibu shtaka la kuongoza kikundi ambacho hakifuati sheria ambacho kilisababisha kifo cha askari polisi mmoja Jumatano wiki iliyopita.

Washtakiwa walikana mashtaka na waliachiliwa kwa dhamana, muda mfupi baada ya Dr. Besigye na viongozi wengine kupewa dhamana.

Wafuasi wa kundi hili waliokuwa wamejaa nje ya jengo la mahakama waliimba wakisema kuwa siku moja Rais Museveni na mkuu wa polisi Luteni Jenerali, Kale Kayihura wataondoka madarakani.

Dr. Besigye alipoondoka mahakamani hapo, alipanga kutembea kwa miguu kuelekea mjini, lakini polisi waliokuwa mahakamani hapo walimuamrisha apande gari lake, wakisema hafai kuandamana na mtu yeyote.

Kiongozi huyo alitii amri ya polisi hao, lakini alipojaribu kwenda mjini mabishano yalianza tena, kati yake na polisi. Polisi waliziba barabara aliyotaka kutumia na kumuamrisha kutumia njia nyingine hadi ofisini kwake.

Watu wengine waliokamatwa Jumatano wiki iliyopita ni raia tisa ambao wamekuwa rumande hadi Jumatano wiki hii na walitarajiwa kufikishwa mahakamani,lakini hawakuonekana. Wanakabiliwa na shtaka la kumuua askari polisi. Hakimu wa mahakama ya barabara ya Buganda aliwaamrisha maafisa wa magereza wawafikishe washukiwa hao mahakamani Ijumaa ya wiki hii.

Dr. Besigye na viongozi wane wengine wanatarajiwa kurudi tena mahakamani tarehe 17 mwezi ujao.

XS
SM
MD
LG