Wakuu wa nchi za Afrika wameanza mkutano wao mjini Addis Ababa huku wakikabiliwa na maswala mbali mbali ya kiusalama, kuanzia mapigano katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo hadi usalama katika nchi ya Mali.
AU pia inakabiliwa na shughuli ya kupata kiongozi mpya wa Umoja huo baada ya kushindwa kufanikisha shughuli hiyo katika mkutano uliopita.
Baraza la Usalama la AU ambalo lilikutana kabla ya kuanza kwa mkutano wa wakuu wa nchi limesema kuongezeka kwa nguvu za wanamgambo wa kiislamu kaskazini mwa Mali kunatishia usalama wa eneo zima la magharibi ya Afrika.
Kati ya wanaogombea uongozi wa AU ni mkuu wa sasa wa umoja huo, Jean Ping wa Gabon na Bi Nkosazana Dlamini-Zuma wa Afrika Kusini.
Mkutano huo pia unatazamiwa kuzungumzia kwa kina mgogoro wa Congo. Rais Salva Kiir wa Sudan Kusini na Omar al-Bashir wa Sudan wanatazamiwa kukutana kando ya mkutano huo kujadilia mgogoro baina ya nchi zao.